Monday, November 30, 2009

USALAMA WA TAIFA NI LAZIMA UBADILIKE, KAMA TUNATAKA TUSALIMIKE! – Sehemu ya 1

Na. M. M. Mwanakijiji


Usalama wa taifa wa nchi yoyote ile duniani ndiyo kinga ya mwisho dhidi ya tishio lolote la uhuru wa taifa hilo. Nitarudia tena kauli hii. Usalama wa taifa wa nchi yoyote ile duniani ndiyo kinga ya mwisho dhidi ya tishio lolote la uhuru wa taifa hilo. Usalama ya usalama wa Tanzania ndiyo kinga ya mwisho ya uhuru wetu na wakati wowote ule idara hiyo inapokuwa katika shaka, shuku, kutokuaminika, wasiwasi, kudhaniwa, tuhuma, au madai hasi basi uhuru wetu uko matatani.

Wengine wanafikiria uhuru wetu unalindwa na Jeshi la Wananchi au na Polisi, hawa ni watekelezaji wa kile ambacho usalama wa taifa umefanya. Pasipo usalama wa taifa kufanya kazi yake vizuri basi vyombo vya ulinzi vinajikuta vinafanya kazi ngumu zaidi ya kutulinda kwani kinga ya mwisho ya usalama wetu iko matatizoni. Bila ya idara yenye nguvu ya usalama wa taifa kazi ya ulinzi wa taifa inakuwa ngumu zaidi kuliko inavyopasa.

Uhuru wa nchi yoyote duniani unaenda sambamba kabisa na uwezo wake katika mambo ya kijasusi.

Ninapozungumzia Usalama wa Taifa ninazungumzia kundi la watu ambao kutokana na nafasi zao wamepewa jukumu la kukusanya, kuchambua, na kuamua juu ya hatua mbalimbali za kuchukuliwa juu ya taarifa za kijasusi ambazo zinatishia maslahi ya taifa letu. Ninazungumzia wale wenye jukumu la kuhakikisha kuwa mipango yoyote, njama yoyote, na mikakati yoyote ya watu wasiotutakia mema inagundulika mapema kabla haijatekelezwa na hatua za kujibu mashambulizi au kuadhibu zinachukuliwa mara moja. Ni watu ambao jukumu lao kubwa ni kutambua taarifa za kijasusi na kuchukua hatua mara moja za kuzuia kitu chochote, mtu yeyote au jambo lolote kuingilia uwepo wa Taifa letu huru, usalama wa watu wake, na usalama wa maslahi yake mahali popote duniani.

Kati ya mambo ambayo yamo moyoni mwangu kwa muda mrefu sasa ni suala hili la usalama wa taifa. Ninapoangalia mambo kadha wa kadha yanayotokea nchini na ambayo yamekwisha tokea nimejifunza mambo fulani ambayo naamini ni muhimu kuwashirikisha ili tuweze kuelewa vita hii dhidi ya ufisadi kwa muda mrefu ujao haitakuwa na mafanikio bila ya kuboresha vyombo kadhaa na cha kwanza miongoni mwao ni Usalama wa Taifa (UwT).

Nimeshaandika mara kadhaa huko nyuma nikiwa mtu wa kwanza kuvunja mwiko wa kuzungumzia usalama wa taifa hadharani na kwa kina, mwiko ambao ninaendelea nao katika sehemu hii ya kwanza ya mabadiliko ya lazima ya “Idara” kama Watanzania tunataka tusalimike. Ningekuwa na uwezo ningewaweka chini wana usalama wote na kuwapatia somo hili la bure ambalo ningedai ni la lazima kabla ya mtu yeyote kula kiapo cha utumishi!

Kwanini mabadiliko ni lazima?

Umuhimu wa kutaka kusababisha mabadiliko ndani ya idara hii nyeti ni mlolongo wa matukio ya kushangaza ambayo kimsingi kabisa yanatishia uhuru wetu kuliko utawala wa kikaburu au mvutano wa mataifa ya Magharibi na Mashariki wakati wa Vita Baridi. Matukio ambayo tunayaita ni “ufisadi” msingi wake na kutokea kwake kumekuja sababu ya kulegalega na kuyumbayumba kwa idara hii nyeti.

Kinachonitisha zaidi ni kuwa hakuna mtu ambaye yuko tayari kuzungumzia mabadiliko haya na kuanza kuyataka yafanyike na hivyo kuendeleza woga wa kutojadili idara hii huku madhara yakiendelea kutokea. Ni sawa na kuogopa kuzungumza au kujadili walinzi wa jengo letu wakati tunaona tunashambuliwa wakati kuna watu wanalipwa kutulinda.

Hivyo, kama kweli tunataka kuushinda ufisadi na kujenga taifa lenye kufuata kweli misingi ya sheria, utawala wa demokrasia na siasa safi hatuna budi kuboresha idara ya usalama wa taifa, kuiimarisha na kuweza kuijenga ili iweze kukabiliana na changamoto za dunia ya leo. Hivyo, kama kweli tunataka kusalimika huko mbeleni hatuna budi kuboresha idara hii ambayo kiukweli kabisa ni moyo wa taifa letu.

Falsafa ya Usalama wa Taifa

Tunaweza kuigawa historia ya falsafa inayoongoza idara yetu ya Usalama wa taifa katika sehemu kubwa tatu ambazo sitaziangalia kwa undani sana (nitawaachia wengine waje kufanya kazi hiyo). Kuna Kipindi cha 1961-1970, kipindi cha 1970-1985, na kipindi cha 1996-Sasa. Vipindi vyote hivi vimeakisi katika utendaji kazi wa idara hii na kwa namna fulani vinaingiliana.

Kipindi cha 1961-1970 (Miaka ya majaribu- Trial Years)

Wakati huu wa historia tulikuwa tunakabiliwa na changamoto kubwa kadhaa ambazo zilitishia uwepo wa taifa letu na uhuru wetu kwa ujumla. Kilikuwa ni kipindi kigumu zaidi kuongoza. Kwanza, ni kwa sababu nchi yetu ndio imepata uhuru wake na kuwa Jamhuri lakini ikiwa na wataalamu wachache na maafisa wachache wa Usalama wa Taifa ambao walikuwa wamesomea kazi hii. Kilichotegemewa zaidi wakati ule ni ile tunu ya “uzalendo” ambayo watendaji wa kwanza wa serikali yetu iliwaongoza kwani hakukuwa na kitu cha aibu kama kushindwa kulinda uhuru ambao taifa limeupata.

Mapinduzi ya Zanzibar, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, na Maasi ya Jeshi ya mwaka 1964 yalikuwa ni kilele cha udhaifu mkubwa na wakati huo huo somo kubwa zaidi la kuelewa jukumu la idara ya usalama wa taifa (wakati huo ikiwa kama chombo kilichojulikana kuwepo bila kuwa idara iliyojulikana dhahiri). Mambo hayo makubwa yalionesha uwepo wa haja ya kuwa na usalama wa taifa uliokomaa, kusambaa na kufanya kazi kwa nguvu zote:

a. Kulinda serikali iliyo madarakani

b. Kumlinda Rais na tishio lolote dhidi ya nafsi yake na ofisi yake

c. Kulinda Nchi kutoka kwa maadui wa nje (hasa Utawala wa Kikaburu wa Afrika ya Kusini)

Hivyo kipindi hiki kwa kweli kilikuwa na matukio ya kushtua na mengine yaliyotokana na uwoga mkubwa hasa baada ya Uasi wa Jeshi. Jambo hili siyo geni kwa nchi changa. Hata Marekani baada ya kupata uhuru wake kwa njia ya Mapinduzi dhidi ya Himaya ya Mwingereza viongozi wake walikuwa na jukumu kubwa sana la kuhakikisha kuwa wanaulinda uhuru huo kwa kuwa na watu wa usalama wa taifa waliokuwa na uwezo na nyenzo za kuilinda nchi yao.

Kama Tanzania chini ya Mwalimu ilivyofanya makosa ya hapa na palekatika usalama wa taifa mwanzoni mwa jamhuri yetu ndivyo hata Marekani taifa lililoundwa kwa misingi ya usawa wa watu wote lilifanya makosa katika sehemu hiyo nyeti, makosa ambayo miaka karibu zaidi ya 200 baadaye Marekani ilifanya tena na kuligharimu taifa hilo lenye nguvu zaidi duniani matukio ya Septemba 11. Na baada ya hapo Wamarekani wakajikuta wanalazimika kuangalia tena sekta nzima ya ukusanyaji wa habari za kijasusi na suala la usalama wa taifa.

Machafuko ya Rwanda na Burundi mwanzoni mwa miaka ya sitini, mauaji ya Lumumba n.k vyote vilimfanya Mwalimu na uongozi wetu wa awali kuwa na wasiwasi (nervous) na wakati mwingine woga usio na msingi (paranoid) kwa mtu yeyote ambaye alikuwa akionesha dalili ya kuipinga serikali au kuwa mkosoaji sana. Ni njia pia iliyofuatwa na Dr. Hastings Banda wa Malawi na baadhi ya viongozi wa mwanzo wa Afrika na hata sehemu nyingine duniani.

Hivyo, kuangalia idara hii na kufanya mabadiliko siyo jambo la ajabu au mwiko. Hivyo, kipindi hicho cha mwanzo kilikuwa cha mafanikio makubwa lakini pia kikiwa na changamoto ambazo zimeandikwa katika kurasa zisizofutika za historia. Masuala ya kina Kambona, Hanga, kina Bibi Titi Mohammed, n.k yote yanahusiana moja kwa moja na mafanikio na mapungufu ya Idara hii.

Ninaamini miaka ya mwanzo ya nchi yetu taifa letu lilikabiliwa na tishio la ndani zaidi kuliko ya nje na jukumu la kwanza la utawala uliokuwepo ni kuhakikishia kuwa Taifa letu halisambaratiki.

Kipindi cha 1970-1985 – Miaka ya Utukufu (glory years)

Kwa kipimo kikubwa ninaamini Usalama wetu wa taifa ulifanya kazi kubwa zaidi na ya kukumbukwa katika miaka hii 15. Ni miaka ambayo kwanza sheria tuliyoirithi kwa mkoloni ya “Official Secrets” ilifutwa na badala yake sheria ya Usalama wa Taifa ya Mwaka 1970 iliingizwa na kuongoza shughuli za usalama wa taifa.

Tishio kubwa la wakati huu pamoja na matishio ya ndani (halisi au ya kudhaniwa) ni matukio nje ya Tanzania. Kuingia kwa Idi Amin madarakani nchini Uganda na kuendelea kwa majirani zetu kukaliwa na wakoloni kama huko Msumbiji na Zimbabwe na kuendelea kwa utawala wa kikaburu Afrika ya Kusini vilikuwa ni tishio kwa serikali zote za kusini mwa Afrika ambazo zilikuwa zimekwishapata uhuru wake.

Uamuzi wa Tanzania kuongoza harakati za ukombozi Kusini mwa Afrika na kukubali kutumiwa kwa ardhi yake na vikosi vya wapigania uhuru vililifanya taifa letu kuwa kama mnyama aliyewekwa alama na wawindaji, adui wa wakoloni, makaburu alikuwa wazi mbele yao.

Ni kutokana na ukweli huo sheria hiyo ya mwaka 1970 iliingiza katika ibara ya 9 kutambua vikundi vya wapigania uhuru na kulinda maslahi yao. Hivyo katika miaka hiyo na chini ya sheria hiyo Usalama wa Taifa wa Tanzania ulikuwa unatumika siyo kulinda maslahi na usalama wa taifa letu tu bali pia kulinda maslahi na usalama wa vikundi vya wapigania uhuru ambavyo tumevitambua hivyo. Kwa misingi hiyo watu wetu wa usalama walikuwa pia wakiangalia usalama wa SWAPO, ANC, FRELIMO, n.k Hili halikuwa jambo dogo.

Ni kutokana na hili mchango wa watu wetu wa Usalama wa Taifa wakati huo unatambulika hata leo katika baadhi ya nchi na unatambulika kwa shukrani. Ilikuwa ni miaka ya utukufu kwani ni pamoja na mchango wetu huo tuliweza kuchangia siyo damu tu kama wengi wanavyojua katika harakati za ukombozi lakini vile vile mchango wa taarifa na habari za kijasusi zilizowezesha vikundi vya wapigania uhuru kufanikisha malengo mbalimbali ambayo hatima yake kwa kiasi kikubwa ilikuwa ni kupatikana kwa utawala wa kidemokrasia na haki ya usawa kwa watu wote wa Afrika ya Kusini pale Nelson Mandela na wenzake walipofunguliwa kutoka katika shimo la giza la gereza la Kisiwa cha Robin walikotumikia jumla ya miaka ma-mia nyingi.

Kipindi cha 1985-1996 – Miaka ya kukosa mwelekeo (Uncertainty Years)

Mojawapo ya mabadiliko makubwa yalitokea baada ya baba wa taifa kung’atuka katika uongozi wa serikali (1985) na baadaye Uenyekiti wa CCM (1990). Kubadilika huku kwa uongozi kulikuwa pia na changamoto ya namna ya pekee kwa usalama wa Taifa. Miaka mitano ya mwanzo tunaye Rais mwingine ambaye kisheria ndio mkuu wa Usalama wa Taifa, lakini kisiasa nguvu zilikuwa kwa Mwenyekiti wa CCM ambaye katika mfumo wa chama kimoja alikuwa na nguvu ya aina ya pekee.

Hivyo, utii (allegiance) ya watu wa usalama wa taifa kama ilivyokuwa kwa maeneo mengine ilikuwa ni ya kuchanganyikiwa kidogo; Kumtii Mwinyi ambaye alikuwa Rais au Nyerere ambaye alikuwa ni Mwenyekiti wa Chama? Je, Rais akifanya mambo fulani yaliyo ndani ya madaraka lakini yakagongana na mtazamo wa Mwenyekiti wa CCM watu wa chini wasimame na nani?

Matokeo yake Usalama wa Taifa ulianza kugawanyika kwa kufuata mwelekeo wa itikadi; kizazi cha zamani kikiwa kinaongozwa na uzalendo wa aina ya pekee na dhana ya kulinda taifa kama miaka ile ya majaribu na utukufu lakini kizazi kipya cha wasomi zaidi kikianza kuona matundu ya mabadiliko ya kiuchumi aliyoyafungulia Mzee Mwinyi.

Ni katika kipindi hiki tunaweza kuona kwa kiasi cha namna fulani kujipanga kwa vikundi ambavyo leo tunaweza kuviita vya kifisadi. Hili lilikuwa linaanza kuonekana zaidi miaka ile mitano ya utawala wa Rais Mwinyi. Katika kipindi hiki viongozi walianza kukaa kwa kujiamini zaidi na hasa baada ya Baba wa Taifa kuachia uenyekiti wa CCM vile vile na hivyo kumpa nguvu zote za kichama na kiserikali Rais Mwinyi.

Matokeo yake ni kuvunjwa rasmi kwa azimio la Arusha, na kuruhusiwa kwa namna ya pekee vitendo vya kifisadi kuanzia uuzaji wa Loliondo na utoroshaji wa dhahabu. Kipindi hiki kwa baadhi ya watu kilikuwa ni cha neema kwani yeyote aliyetaka alipata endapo tu alicheza karata zake vizuri.

Baada ya Afrika ya Kusini kupata utawala wa kidemokrasia na vyama vya ukombozi kutambulika kama vyama vya kisiasa na Tanzania kupunguziwa jukumu la kulinda maslahi ya vyama hivyo, watu wetu wakawa hawana tishio kubwa zaidi la kuangalia zaidi ya kuangalia usalama wa viongozi na serikali iliyoko madarakani na dola (state).

Hii ilikuwa ni miaka ya kukosa mwelekeo kwa sababu adui yetu wakati huo alikuwa ni nani? Vita baridi vilikuwa vimekoma kwa kusambaratika kwa Shirikisho la Kisovieti la Urusi (USSR) na kuibuka kwa Marekani kama Taifa pekee lenye nguvu zaidi duniani; Afrika ya Kusini imerejea katika utawala wa demokrasia, na wimbi la mageuzi ya kisiasa lilikuwa linasambaa katika Afrika. Siyo wimbi la mapinduzi ya kijeshi bali mabadiliko ya kisiasa kwa njia za kidemokrasia.

Je, watu wetu wa Usalama walikuwa wanalinda maslahi ya nani zaidi? Kwa wachache kilikuwa pia ni kipindi cha kuanza kushiriki katika vitendo vya kifisadi. Katika ripoti zinazokuja tutaangalia baadhi ya matukio ya wakati huu ambayo yalifungulia mlango wa ufisadi kuanzia Ikulu hadi nyumba ya mwisho kabisa karibu na shamba la kijiji!

Kipindi cha 1996-Sasa – Miaka ya Aibu (Shameful Years)

Sasa hivi tunaishi katika kipindi cha aibu. Kipindi ambacho nikisikia mtu anajiita mtu wa “usalama” nasikia kukereka (nilitaka nitumie neno jingine hapa!). Si kwamba ninawahukumu wote kuwa wameacha wito wao bali kuna kikundi kati yao ambacho kimeacha suala la usalama wa taifa na badala yake kimebakia kwenye “usalama wa wanasiasa”! Hiki siyo kitu kimoja.

Kundi hili limegeuza “usalama wa taifa” na kuwa usalama wa “chama tawala” na hofu yangu ni kuwa wanatumia muda mwingi kufikiria Tanzania katika mwanga wa siasa za vyama na kusahau kuangalia Tanzania kama jamhuri. Wakati wowote usalama wa taifa unapoacha kuangalia taifa na kuhamisha macho yao kwenye vitu vingine, basi usalama huo wa taifa unakuwa umepotea na ni mabadiliko ya haraka na ya lazima ndiyo yanaweza kurejesha huko.

Miaka hii ya aibu ilianza kwa kuundwa kwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa sheria namba 15 ya Usalama wa Taifa ya 1996 iliyosainiwa na Rais Benjamin Mkapa Januari 20, 1997 kuwa sheria.

Sheria hii ndiyo ilirasmisha uwepo wa idara ya usalama wa taifa na kuwatoa gizani watu waliokuwa wanajulikana uwepo wao lakini pasipo kuonekana. Iliweka msingi wa utendaji kazi wa idara hiyo, utaratibu wake hadi viapo vya wana usalama. Kwa juu juu sheria hii ukiangalia kwa haraka unaweza kufikiri ilikuwa ni nzuri. Kitu kizuri pekee ambacho naweza kusema kiko ndani ya sheria hii (zaidi ya vipengele vyake kadhaa) ni kujenga taasisi rasmi ya usalama wa taifa.

Hata hivyo, mambo mengine yaliyomo katika sheria hiyo ni mambo ambayo mtu yeyote aliyesomea mambo ya ujasusi anaweza kujikuta anahuzunika kwani sheria hii imefungua mwanya wa ufisadi wa kimataifa na kuwafunga kwa minyororo watu wetu wa usalama. Ni sheria mbayo kama ningekuwa na uwezo ningeibadilisha siku ya kwanza Rais Kikwete anaingia madarakani.

Ninaamini kwa moyo wangu wote kuwa sheria hii ilifikiriwa, kutungwa, na kubarikiwa na miungu ya mafisadi! Mtu mwenye akili timamu mwenye kulipenda taifa lake na kujali maslahi ya taifa lake asingeweza kuivumilia iwepo kwa zaidi ya saa moja! Ni sheria inayotishia usalama wetu wa taifa na natumaini kuna mtu ataamka na kutaka kuifanyia mabadiliko ya haraka kama tunataka tusalimike.

Sheria hii kwa maoni yangu ni sawa na mtu ambaye ameamua kulinda mifugo yake, kajenga uzio mkubwa na kaweka lango kuu. Kaajiri na walinzi na kutoa maelekezo ya walinzi kuwa waangalifu. Tatizo ni kuwa baada ya kufanya haya yote, mtu huyo hakuweka lango la kuzuia watu kuingia na hivyo kuacha uzio ukiwa na uwazi huku yeye mwenye akijivunia kuwa amejenga “uzio” mkubwa sana! Anapoamka asubuhi anakuta nusu ya mifugo imetoweka na mlinzi akisimama upande mwingine wa jengo!

Hatuwezi kwenda mbele kama taifa na hasa kukabiliana na changamoto zilizoko mbele yetu na hasa adui yetu mpya ambaye leo hii anatuchezea kama kucheza shere kwa sababu ya udhaifu wa sheria hii. Ni sheria ambayo wapiganaji wa CCM ningetamani wasema tunataka kuifanyia mabadiliko kwani ni mojawapo ya vitu vinavyotengeneza mfumo wa utawala wa kifisadi.

Tutaingalia sheria hiyo ya TISS (Tanzania Intelligence and Security Service) katika sehemu ya pili ya hoja hii. Tutafanya hivyo baada ya kuangalia ni adui gani sasa hivi anayetishia uhuru wetu zaidi na kwanini ni adui wa hatari zaidi kuliko uvamizi wa Nduli au njama za Makaburu wa Afrika ya Kusini.

Usikose sehemu ya pili.

Niandikie: mwanakijiji@mwanakijiji.com

Friday, November 27, 2009

Ziwa Ngozi linalodaiwa kuhamishwa kwa jiwe la moto

Na Thobias Mwanakatwe

Tanzania ni nchi iliyobahatika kuwa na maziwa mengi hata hivyo kila ziwa lina historia yake jinsi lilivyojitokeza kwa maana ya chanzo chake.

Ziwa Ngozi lililoko Rungwe ni moja ya maziwa ambayo wenyeji huogopa kulitembelea kutokana na imani walizonazo. Mwandishi Wetu, Thobias Mwanakatwe, anaandika zaidi.

Yapo maziwa au maeneo ambayo ukianza kusimuliwa historia yake unaweza kabisa ukakata tamaa hata kulitembelea hasa kutokana na maajabu yaliyopo katika ziwa hilo.

Mojawapo ya maeneo yenye historia ya maajabu ni ziwa Ngozi lililopo katika kijiji cha Mbeye One wilayani Rungwe katika mkoa wa Mbeya.

``Mimi sijawahi kufika huko lakini siwezi kwenda kule kunatisha,`` anasema Uswege Mwakimbete alipoulizwa kama amewahi kufika kwenye ziwa hilo.

Ziwa hilo liko urefu wa mita 150 kutoka kilele cha milima inayozunguka ziwa , ambapo kutoka usawa wa maji kina cha maji ni urefu wa mita 73 na ukubwa wa eneo lenye maji ni kilomita sita hadi 10 za mraba na lina ukubwa wa kilometa za mraba 3.75.

Wataalam wanaeleza kuwa ziwa hilo limetokana na volkano , limezungukwa na misitu mizuri ya asili ya kitropiki hali nzuri ya hewa na tulivu.

Ili kulifikia ziwa hilo unalazimika kutembea kwa mwendo wa kati ya dakika 45 na saa 1 kutoka kijijini Mbeye One ambacho kipo barabara kuu ya Mbeya-Kyela.

Pia kutoka katika kilele cha milima inayozunguka ziwa hilo unalazimika kushuka kwa zaidi ya dakika 45 huku ukilazimika kushuka kwa kutumia mizizi migumu ya miti ya asili iliyopo katika msitu mnene kwasababu ya mteremko mkali kuelekea katika ziwa hilo.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbeye One, Watson Mwakalinga anasema kuwa ziwa hilo liligunduliwa mwaka 1925 ambapo anasema kuwa ziwa hilo lilihama kutoka katika kijiji cha Mwakaleli wilayani humo baada ya kudaiwa kuwa baada ya kuchomwa na jiwe la moto na wakazi wa kijiji hicho.

Anasema ziwa hilo la maajabu lilichomwa moto na wakazi wa kijiji cha Mwakaleli kwasababu lilikuwa likileta mikosi mingi kijijini hapo ikiwemo watu kufa kila mara hali iliyowalazimu wazee wa kijiji hicho kufanya uchunguzi na kubaini kuwa kunasababishwa na ziwa hilo la Ngozi.

Hata hivyo unapowauliza wataalam wa masuala ya mazingira wanasema kisayansi ziwa haliwezi kuhama.

``Kwa vile ziwa hili halikuwepo pengine wangesema kuwa halikuwepo mpaka volkano hiyo ilipokuwepo lakini ziwa haliwezi kuhama,`` anasema Prof .William Rugumamu , wa Idara ya Jiografia toka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Mwakalinga anasema kuwa maajaabu ambayo yametokana na imani za kishirikina yanayodaiwa kuwepo katika ziwa hilo ni pamoja na watu wanaofika huku kudaiwa kupotea, sauti za vikohozi vya watu wasioonekana pamoja na miujiza ya watu wanaotwanga mahindi lakini hawaonekani.

Anasema mbali ya maajabu mengine ya imani za kishirikina yaliyokuwepo, anasema kuwa ziwa hilo linatabia ya kubadilika rangi ambapo anasema ziwa hilo limekuwa likigeuka rangi mara kwa mara na kuwa na rangi za kijani, bluu, nyeusi na nyeupe.

Anasema kubadilika kwa maji katika ziwa hilo kimsingi wananchi wameshindwa kufahamu kunatokana na nini ingawa waatalam waliowahi kufika kijijini hapo wanadai kunatokana na mabadiliko ya hali ya hewa ya eneo hilo.

Prof. Rugumamu anasema hali ya kubadilika rangi kwenye ziwa Ngozi siyo kitu cha ajabu kwani ni hali inajitokeza kwenye maji ya bahari ambapo anasema wakati mwingine huweza kuonekana rangi ya bluu au rangi ya upinde kutegemeana na hali ya jua.

`Kwenye maji ya bahari hali ya maji kubadilika ni jambo la kawaida pengine watu hawawi makini kuangalia tu,`` anasema Prof. Rugumamu ambaye ni mtaalam wa masuala ya mazingira na hali ya udongo.

Hata hivyo unapofika eneo hilo misitu inayozunguka ziwa hilo ina hali nzuri pamoja na baadhi ya wanyama wakiwemo chui na nyani, ingawa ni nadra sana kuwaona chui katika misitu hiyo kwa kuwa wanajificha na hawajawahi kuleta madhara kwa binadamu.

Anasema kutokana na maajabu hayo, wakazi wa kijiji hicho walikuwa wakiogopa kabisa kufika katika ziwa hilo kutokana na maajabu hayo yaliyokuwa yakisemwa.

Mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Mbeye 1, George Mbepe (65), anasema awali walikuwa wanahofia kufika katika ziwa hilo kutokana na madai ya kuwapo kwa imani za kishirikina.

``Kulikuwa na imani kuwa mtu akija huku atasikia vikohozi vya watu wasioonekana huku wengine wakitwanga mahindi, lakini hawaonekani,`` alisema na kuongeza kuwa imani hizo zilisababisha watu wasifikirie kwenda katika ziwa hilo .

Hata hivyo anasema, kuwa kutokana na maji hayo kuonekana yanafaa, yamekuwa yakitumiwa kama mradi na vijana ambao wamekuwa wakiuza kati ya shilingi 300 na 500 kwa lita.

Wakazi wa Kijiji hicho, wanaamini maji ya ziwa hilo hutumika kama dawa kwa ajili ya kutibu watoto ambao wamekuwa wakistuka nyakati za usiku na kwamba pindi wanaponywesha maji hayo hali hiyo inakoma mara moja.

Prof .Rugumamu anasema kuwa hakuna maelezo yoyote ya kisayansi ya Ngozi kuwa na uwezo wa kuponya magonjwa lakini anasema wenyeji kwenye maji mengi yanayotokana na volkano wamekuwa na imani za aina hiyo.

``Hata sehemu nyingi ambako yanatoka maji moto yanayotokana na volkano watu wanaamini hiyo lakini hiyo ni imani tu, anasema .``

Ziwa hilo liliwahi kupandikizwa samaki aina ya perege mwaka 2001, hata hivyo hadi sasa hawajafanikiwa kuvua samaki hata mmoja kutokana na ukosefu wa vifaa vya uvuvi pamoja na ugumu wa kufika katika ziwa hilo .

Hata hivyo imani hizo za kishirikina za wakazi wa Kijiji hicho zilifikia tamati mwanzoni mwa mwaka huu baada ya timu ya watafiti wa Kimataifa kutoka nchi za Ufaransa, Uingereza na Ubelgiji kufanikiwa kufika katika ziwa hilo na kufanikiwa kuingia ndani ya ziwa hilo na kuchota udongo kwa ajili ya kufanya utafiti wa kisayansi kuhusiana na ziwa hilo pamoja na mazingira yanayolizunguka.

Watafiti hao walibaini kuwa ziwa hilo lina umri wa zaidi ya miaka 40,000.Ingawaje wataalam wengine wanasema kuwa ziwa hilo linaweza kuwa lilikuwepo hata miaka milioni 2 iliyopita.

Kuna baadhi ya watalii wamekuwa wakitembelea ziwa hilo ambapo hulipia kiasi cha Sh 2,000 kwenda kuliona .

Hata hivyo baadhi ya wananchi wanasema kuwa kiasi kinachotozwa cha sh.2,000 hakitoshi bali wangetozwa zaidi.

``Watalii walitakiwa kutozwa shilingi 10,000 na watanzania walipe shilingi 2,000 ili mapato yatokanayo na shughuli za utalii yaweze kutumika kwa shughuli za maendeleo katika Kijiji na wilaya,`` anasema Jackson Mwakabuta,mkazi wa kijiji hicho.

Mwakabuta anasema kuwa idadi ya watalii wanaotembelea vivutio vya utalii wilayani humo haitoshelezi, ambapo alisema kuwa kuna haja ya kufanyika kwa juhudi za makusudi kutangaza vivutio vilivyopo nchini pamoja na kuwahamasisha Watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya utalii badala ya kuwategemea wageni tu.

Mbali ya ziwa hilo kukosa watalii wanaotembelea kuangalia vivutio vilivyopo, pia wakazi wa Kijiji cha Mbeye One, wameshindwa kuendesha shughuli za uvuvi kutoka katika ziwa hilo kutokana na ukosefu wa vifaa vya uvuvi pamoja na ugumu wa kufika katika ziwa hilo la shimo ambalo limezungukwa na milima.

Wananchi hao wanaiomba serikali iwasaidia kupata boti itakayotumika kwa shughuli za uvuvi katika ziwa hilo, ambapo alisema kuwa kuanza kwa shughuli za uvuvi kutasaidia kukuza uchumi wa kijiji hicho na hivyo kuinua maisha ya wananchi .

Mwambata wa Ubalozi wa Ufaransa nchini, Dk. Raymond Latest ambaye alikuwa pamoja na timu ya utafiti wa ziwa hilo anasema kuwa wilaya ya Rungwe ina vivutio vizuri vya utalii kuliko mkoa wa Arusha lakini havifahamiki kutokana kwa kutotangazwa.

Anasema awali kabla hajafika nchini, alikuwa akiifahamu zaidi nchi ya Kenya ambayo imekuwa ikijitangaza zaidi kwenye utalii, lakini alipofika nchini akagundua kuwa Tanzania ina vivutio vingi vya utalii ikiwamo misitu ya asili kuliko nchi yoyote ya Afrika Mashariki.

Dk.Latest anasema vivutio hivyo vikitangazwa vizuri vitaweza kuchangia kukuza pato la Taifa kupitia sekta ya Utalii.

Akilizungumzia ziwa Ngozi, Dk. Latest alisema kuwa amevutiwa na ziwa hilo lililozungukwa na milima na kuonekana lipo shimoni pamoja na kuzungukwa na misitu ya asili, ambapo alisema kuwa atahakikisha anaitangaza wilaya ya Rungwe ili iweze kufikiwa na watalii wengi kutoka nchini Ufaransa na watalii waweze kujionea maajabu ya wilaya hiyo.

Kiongozi wa timu ya watafiti, Dk. David Williamson kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anasema hiyo ilikuwa mara yao ya kwanza kufika katika ziwa hilo kwa lengo la kufanya utafiti ili kujua umri wa ziwa hilo, mabadiliko ya hali hewa na mazingira pamoja na kufahamu volkano ndogo ya mwisho ililipuka lini. Na kama maji ya ziwa hilo yanafaa kwa matumizi ya binadamu.

Dk. Williamson anasema kuwa ziwa ngozi ni moja kati ya maziwa 10 ya volkano yaliyopo wilayani Rungwe ambayo wanafanyia utafiti wa kisayansi, aliyataja maziwa mengine kuwa ni pamoja na Ndwati, Kisiba, Chungululu, Ikapu, Itamba, Asoko, Ilamba, Kingili, Katubwi na Itende.

Utafiti wao unajumuisha uchukuaji wa vumbi na tope lililopo chini ya ziwa hilo vitu ambavyo vitasaidia katika utafiti wao.

Katika utafiti wao wa awali waligundua kuwa kina cha maji katika ziwa hilo kinazidi kupungua kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, mmonyoko wa udongo na kwamba hali hiyo inahatarisha uwepo wa ziwa hilo kwa miaka ijayo.

Akieleza sababu za kuchukua tope lililochini ya ziwa hilo , alisema kuwa wanaamini kuwa tope lililoganda ndani ya maji linakuwa na mkusanyiko wa tabaka mbalimbali za taka, udongo na kwamba kiasi wanachochukuwa kitawawezesha kujua mambo muhimu wanayoyahitaji katika utafiti wao.

Mtafiti mwingine kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ,Edister Abdallah anasema kuwa utafiti huo utasaidia wakazi wanaosihi kuzunguka ziwa hilo kuendana na mabadiliko ya hali ya hewa hivyo kushiriki katika kuhifadhi mazingira ya eneo hilo na wilaya ya Rungwe na hivyo kufanya uwepo wa ziwa hilo kuwa endelevu.

Anasema kuwa juhudi za dhati zinapaswa kuchukuliwa ili kuwajengea wananchi utamaduni wa kutunza mazingira tofauti na ilivyo sasa ambapo wananchi hawaoni wajibu wao wa kushiriki katika kutunza na kuhifadhi mazingira ambayo ni muhimu katika maisha ya mwanadamu na viumbe hai.

Alisema kuwa wananchi wakipatiwa elimu na kujua umuhimu wa kuhifadhi mazingira kila mmoja atatimiza wajibu wake kwa kutunza mazingira.

Anaongeza kuwa ukosefu wa elimu umekuwa ukisababisha wananchi wengi washiriki katika uharibifu wa mazingira bila wao kujua au wengine kuharibu kwa makusudi bila kujua athari za baadaye za uharibifu huo.

Naye Mshauri wa Sekta ya Wanyamapori mkoa, Stanley Munisi anasema mkoa wa Mbeya unao vivutio vingi vya kitaalam, lakini vingi bado havijatangazwa na kwamba hivyo ipo mikakati ya kuanza kuzitangaza.

Vivutio vya Mbeya vina nafasi kubwa kukuza uchumi

Na Mwadishi Wetu



Mh. Profesa Mark Mwandosya akitembelea maporomoko ya Malamba wilayani Rungwe ambayo ni mojawapo ya vivutio kibao vya utalii mkoani Mbeya.

JIJI la Mbeya lina vitongoji vingi vyenye utajiri. Lina vivutio vingi kwa wageni waliopata fursa ya kulitembelea. Mbeya ina safu za milima iliyosheheni rasilimali za urithi tangu zama za kale. Rasilimali hizo ni pamoja na misitu mikubwa iliyo hifadhi wanyama na ndege wazuri wa kuvutia.

Mbeya ni Mkoa ulioandika historia ya maajabu katika bara la Afrika na ulimwenguni, tangu kilipodondoka kimondo. Kimondo hicho kilidondoka katika Wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya.Vivutio vingine vinavyoipamba Mbeya ni mabwawa yenye matukio ya maajabu, kwa mfano bwawa lililopo Masoko, jirani na kilele cha Mlima Rungwe.

Pia, Ziwa Ngozi na Daraja la Mungu ni baadhi ya vivutio vinavyotengeneza historia ya pekee ya Mbeya na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Ziwa Nyasa ni kivutio kingine, ambapo watu kutoka mataifa mbalimbali hufika kujionea ziwa hilo lenye hadhi kubwa katika bara la Afrika.

Wageni mbalimbali hufika wilayani Kyela kujionea mandhari ya ziwa hilo, ambalo ni la tatu kwa ukubwa barani Afrika. Ziwa hilo pia lipo katika nchi tatu za Malawi, Msumbiji na Tanzania. Wananchi wa nchi hizo na wageni wengine, hunufaika na Ziwa Nyasa kwa uvuvi wa samaki na viumbe wengine waishio majini, kwa ajili ya chakula na biashara.

Ziwa hilo pia limerahisisha usafiri kati ya bandari za Mbamba Bay na Itungi. Lakini, jambo kubwa la kujivunia katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ni kuwapo kwa pango la Matema na Hoteli ya Matema. Hoteli hiyo ya ufukweni imeboresha mazingira ya ufukwe wa Matema na kuufanya kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni wanaofika hapo.

Matema ni eneo tulivu, lenye mandhari mwanana na mimea ya rangi ya kijani kibichi, iliyopambwa na safu za milima. Milima hiyo imesheheni misitu, inayopatikana ndege wazuri wa angani. Wageni wanaotembelea hotelini hapo, huvutiwa na mandhari hiyo. Hoteli ya Matema ipo katika mwambao wa Ziwa Nyasa. Eneo hilo lilikuwa pori, lakini sasa limegeuka kuwa lulu kwa watu wa makabila tofauti ya ndani na nje ya nchi.

Eneo hilo limejaa utulivu na lina sauti za ndege. Baadhi ya wageni waliowahi kutembelea eneo hilo, wanadiriki kulifananisha na bustani ya Edeni. Kanisa la Uinjilisti lenye makao yake makuu Mbalizi, Mbeya Vijijini, ndicho chanzo cha kuwapo kwa hoteli hiyo, maarufu kama Matema Lake Shore Resort.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Kanisa hilo, Mchungaji Marcus Lrhner, anasema kuwa Kanisa la Uinjilisti lilifanya utafiti na kugundua kuwa eneo hilo linafaa kuweka vivutio na vivutio hivyo vinaweza kukuza sekta ya utalii nchini. Anasema kumekuwa na mafanikio kutokana na kuwapo kwa kivutio hicho.

Mafanikio hayo yanatokana na juhudi za kanisa hilo, kwa kupitia wafadhili wake, ambao kwa miaka nane sasa wamekuwa wakijitahidi kutunza mazingira. Mchungaji Lehner anasema kwamba utafiti uliofanywa pia ulizingatia kuwapo kwa eneo zuri la kuogelea, lenye mchanga safi na mzuri. Anasema Lake Shore Resort inatoa huduma za kulala na chakula cha asili, kinachoandaliwa kwa muda maalumu (kwa oda).

Pia, ina nyumba mbalimbali zenye jumla ya vyumba 22, ikiwamo vyumba vya kujihudumia (self contained) na vyumba vya vitanda viwili hadi vitano. Zipo pia nyumba za ghorofa, zinazomwezesha mgeni kutazama vizuri ziwa, lilivyo na umbo lake, kabla ya kutumia usafiri wa boti, wa miguu au gari. Huduma hizo pia hupatikana hapo.

Matema ipo katika eneo la Kaskazini, mwishoni mwa Ziwa Nyasa, ndani ya Wilaya ya Kyela. Ziwa lina upana wa wastani kilomita 60 na urefu wastani kilomita 550. Lipo kwenye Bonde la Ufa katika Afrika Mashariki na lina ujazo wa mita 500 kutoka usawa wa bahari. Ufukwe wa Matema unapambwa na safu za mlima Livingstone, wenye urefu wa mita 3,000.

Tutaboreshaje elimu katika shule za serikali?

BY BENJAMIN NKONYA


Chimbuko la maendeleo ya elimu nchini ni matokeo ya michakato ya sheria, falsafa na sera zilizoanzishwa katika vipindi mbalimbali kabla na baada ya uhuru. Baada tu ya kupatikana uhuru mwaka 1961, serikali ilitunga sheria ya elimu namba 83 ya mwaka 1962 iliyofuta sheria ya elimu ya mwaka 1927 ambayo iliruhusu utoaji wa elimu na mafunzo kwa mfumo wa ubaguzi wa rangi, dini na makabila.

Katika sheria hii, serikali iliekeza mitaala, uongozi na ugharamiaji wa elimu na mafunzo ufuate usawa. Azimio la Arusha la mwaka 1967 lilianzisha falsafa ya elimu ya kujitegemea ambayo ilisababisha mabadiliko makubwa katika sera za jumla za kijamii na kiuchumi.

Falsafa hii, ambayo iliasisiwa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ndiyo inaweka dira katika mfumo wetu wa elimu hadi leo, inaweka mkazo katika kuondoa matabaka kwenye utoaji wa elimu, utengano (alienation) kati ya shule na jamii na kusaidia kuondoa kasumba ya wasomi ya kujibagua na kutumia elimu waliyoipata kwa manufaa yao binafsi.

Aidha falsafa hii inaelekeza katika kuunganisha nadharia na vitendo, kwa dhana kuwa elimu isipatikane vitabuni tu bali ijumuishe na ile ipatikanayo kutokana na uzoefu wa kutenda au kufanya kazi ya kuongeza tija.

Ili kuhakikisha kwamba haya yanafikiwa na pia kuhakikisha kwamba wanafunzi wanawajibika na upatikanaji wa mahitaji yao, falsafa hii inaelekeza shule kuwa vituo vya kuzalisha mali ili kuchangia gharama za uendeshaji kwa asilimia ishirini na tano. Pia elimu inayotolewa katika ngazi zote iwe na maarifa na stadi za kumwezesha mhitimu kuishi na kufanya kazi yenye manufaa katika jamii.

Katika kutekeleza falsafa hii, shule karibu zote zilitaifishwa na kuendeshwa na serikali kuanzia mwaka 1967. Ili kuondoa aina zote za ubaguzi, serikali ilikubali kugharamia elimu katika ngazi zote. Pamoja na hayo, kila shule ilianzisha mashamba ambayo yalikuwa maarufu kama mashamba ya elimu ya kujitegemea. Hali hii ilimfanya mwanafunzi wa Kitanzania kuwa tayari kujitegemea mara tu baada ya kuhitimu mafunzo ya elimu ya msingi. Kwa hakika falsafa hii ilishabikiwa sana na kila Mtanzania.

Pamoja na uzuri wa falsafa hii, kuna changamoto zilizoukabili mfumo mzima wa elimu katika miaka kumi ya utekelezaji wa falsafa hii. Kama wote tunavyofahamu, katika nusu ya pili ya miaka ya 1970, ubora wa elimu yetu ulishuka sana kiasi kwamba serikali iliruhusu walimu wasio na sifa kuanza kufundisha katika shule za msingi.

Changamoto hii iliambatana na ukosefu wa zana za kufundishia na kujifunzia kama vitabu, maabara, maktaba n.k. Sambamba na changamoto hii, ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi halikuenda sambamba na ongezeko la idadi ya vyumba vya madarasa na samani zake, achlia mbali nyumba za waalimu.

Hivyo ililazimu chumba kimoja cha darasa kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi kuliko idadi inayomfanya mwalimu alimudu darasa kiufundishaji. Pamoja na changamoto hizo, hata suala la usimamizi wa elimu nalo lilikuwa gumu kutokana na shule kuwa nyingi katika mtawanyiko wa kijiografia ambao una ufanisi mdogo. Matokeo ya hali hii ilikuwa ni kushuka kwa elimu kwa haraka sana.

Serikali iling’amua changamoto hizi na kutafuta namna ya kuziondoa ili elimu iendelee kutolewa kwa ubora unaotegemewa. Mwaka 1978 Bunge lilitunga sheria mpya ya elimu namba 25 ambayo, pamoja na mambo mengine, iliruhusu watu binafsi, mashirika ya dini, asasi za kiraia na makampuni kuanzisha, kusajili na kuendesha shule.

Kuanzishwa kwa sheria hii kulianza kuonyesha matumaini ya kunusuru ubora wa elimu kwani shule nyingi binafsi zilionyesha mafanikio. Kuna changamoto kadhaa ambazo zilijitokeza katika miaka kumi na tano ya kwanza ya utekelezaji wa sheria hii.

Changamoto hizi zilirekebishwa kupitia sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995. Hivyo mfumo wetu wa sasa wa utoaji wa elimu na mafunzo nchini unaongozwa na sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995 (iliyopata nguvu kutokana na marekebisho ya sheria ya elimu Na. 25 ya mwaka 1978 iliyorekebishwa kwa sheria Na. 10 ya mwaka 1995), sera ya elimu ya ufundi ya mwaka 1996 na sera ya elimu ya juu ya mwaka 1999.

Pamoja na ukweli kwamba shule za serikali zinaendeshwa kwa kodi za Watanzania pamoja na ufadhili mwingi sana kutoka mashirika mbalimbali ya ndani nje ya nchi, elimu yetu, hasa inayotolewa na shule za serikali, bado ina changamoto nyingi sana katika viashiria vya utoaji (input), mchakato (process) na matokeo (outputs).

Baada ya marekebisho hayo na baada ya sekta binafsi kujiimarisha ipasavyo, Watanzania wameendelea kushuhudia kukua kwa haraka sana kwa elimu katika sekta binafsi licha ya ukweli kwamba shule hizi hazina ruzuku yoyote kutoka serikalini. Sasa ni zaidi ya miaka thelathini tangu kuruhusiwa kwa sekta binafsi kuingia katika utoaji wa elimu.

Pengine ingekuwa busara kudurusu sababu hasa za tofauti hizi na kutafuta namna ambavyo elimu yetu katika sekta ya umma inaweza kuboreshwa.

Ni ukweli usionpingika kwamba gharama za uendeshaji katika shule za serikali ni kubwa kuliko gharama katikashule binafsi. Hii inatokana na ukweli wa kiuchumi kwamba kadri mradi unavyozidi kuwa mkubwa ndivyo ufanisi kwa kila shilingi inayotumika unavyozidi kushuka. Hali hii inakabili vilivyo shule zetu za serikali.

Moja ya viashiria vya kushuka kwa ufanisi ni hii hali ya waalimu kuwa na malalamiko yasiyoisha kuhusu mapunjo wanayopata katika malipo yao, baadhi ya wanafunzi kuvuka madarasa na vidato bila kujua kusoma na kuandika, kukosekana kwa maabara, maktaba, vitabu na vifaa vingine vya kujifunzia na kufundishia na mambo mengine yanayofanana na hayo.

Sababu nyingine za kudorora kwa elimu katika shule za serikali ni kuingiliwa kupita kiasi na wanasiasa. Utakuta taarifa ya wakaguzi inaonyesha kabisa kwamba shule fulani haitakiwi kusajiliwa kutokana na kutotimiza baadhi ya vigezo vya usajili. Pamoja na taarifa hizo, utakuta mwanasiasa anaingilia kati na kulazimisha shule hiyo isajiliwe.

Hivyo hata uendeshaji wake huenda kisiasa siasa tu bila kujali vigezo muhimu vya uendeshaji wa shule. Utakuta shule ya serikali imesajiliwa lakini haina hata kitabu kimoja wala maabara. Itakuwa ni ajabu isiyo kifani kukuta shule kama hii ikitoa elimu bora.

Hali ni tofauti kabisa katika shule binafsi. Shule hizi husimamiwa na kwa ukaribu sana. Shule hizi hukaguliwa na kusajiliwa baada ya kutimiza vigezo vyote vya usajili. Huwezi kukuta shule binafsi inasajiliwa wakati haina maktaba yenye vitabu au maabara zenye vifaa vyote. Hata baada ya usajili, wakaguzi hufika katika shule hizi mara kwa mara kuangalia kama kila kigezo cha utoaji wa elimu kinazingatiwa.

Sambamba na hili, utakuta mmiliki wa shule hizi anafuatilia kwa karibu sana kila kinachoendelea shuleni na kuhakikisha wanafunzi wake wanapata huduma zinazotakiwa.

Kwaujumla wake ni kwamba shule binafsi huendeshwa kwa kufuata mahitaji ya wateja wake na kutimiza masharti yote yanayowekwa na serikali.

Kurunzi haioni kama itatosha tu kukosoa bila kutoa mapendekezo ya ubereshaji. Njia ya kwanza ni kuondoa siasa katika uendeshajiwa usajili na uendeshaji wa shule.

Hii inaweza kufikiwa kwa njia ya kuifanya idara ya ukaguzi kuwa wakala inayojitegema badala ya hali iliyopo ya kuwa idara katika Wizara Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Itakuwa ni ajabu ya ngariba kujitia suna mwenyewe kama kitengo hiki kitatenda haki hasa wakati shule ya serikali inapofanya makosa.

Njia ya pili ni kuweka ushirikiano kati ya wamiliki wa shule binafsi na serikali ili kuondoa tatizo la kushuka kwa ufanisi wa usimamizi unaotokana na kukua kwa idadi ya shule zinazosimamiwa na mmiliki mmoja.

Katika hali hii, mmiliki wa shule binafsi anaweza kuwekwa kuwa meneja wa shule ya serikali (hasa hizi za kata) iliyo karibu naye. Kama meneja, atahakikisha kwamba anashirikiana na bodi ya shule katika kuhakikisha kwamba shule hii ya kata inatoa elimu bora kama ilivyo shule yake.

Elimu ni mali ya umma na inatakiwa kugharamiwa na umma hata kama inatolewa na shule/chuo binafsi. Kurunzi inaamini kabisa kwamba, tukilizingatia hili, tutakuwa tumekata kabisa mizizi yote ya ufisadi dagaa, papa na nyangumi na tutakuwa tumeenzi na kuhuisha fikra sahihi za Baba yetu wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Thursday, November 26, 2009

Vivutio vya Mbeya vina nafasi kubwa kukuza uchumi

Na Mwadishi Wetu



Daraja la Mungu lililopo Wilayani Rungwe


JIJI la Mbeya lina vitongoji vingi vyenye utajiri. Lina vivutio vingi kwa wageni waliopata fursa ya kulitembelea. Mbeya ina safu za milima iliyosheheni rasilimali za urithi tangu zama za kale. Rasilimali hizo ni pamoja na misitu mikubwa iliyo hifadhi wanyama na ndege wazuri wa kuvutia.

Mbeya ni Mkoa ulioandika historia ya maajabu katika bara la Afrika na ulimwenguni, tangu kilipodondoka kimondo. Kimondo hicho kilidondoka katika Wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya.Vivutio vingine vinavyoipamba Mbeya ni mabwawa yenye matukio ya maajabu, kwa mfano bwawa lililopo Masoko, jirani na kilele cha Mlima Rungwe.

Pia, Kisiwa Ngozi na Daraja la Mungu ni baadhi ya vivutio vinavyotengeneza historia ya pekee ya Mbeya na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Ziwa Nyasa ni kivutio kingine, ambapo watu kutoka mataifa mbalimbali hufika kujionea ziwa hilo lenye hadhi kubwa katika bara la Afrika.

Wageni mbalimbali hufika wilayani Kyela kujionea mandhari ya ziwa hilo, ambalo ni la tatu kwa ukubwa barani Afrika. Ziwa hilo pia lipo katika nchi tatu za Malawi, Msumbiji na Tanzania. Wananchi wa nchi hizo na wageni wengine, hunufaika na Ziwa Nyasa kwa uvuvi wa samaki na viumbe wengine waishio majini, kwa ajili ya chakula na biashara.

Ziwa hilo pia limerahisisha usafiri kati ya bandari za Mbamba Bay na Itungi. Lakini, jambo kubwa la kujivunia katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ni kuwapo kwa pango la Matema na Hoteli ya Matema. Hoteli hiyo ya ufukweni imeboresha mazingira ya ufukwe wa Matema na kuufanya kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni wanaofika hapo.

Matema ni eneo tulivu, lenye mandhari mwanana na mimea ya rangi ya kijani kibichi, iliyopambwa na safu za milima. Milima hiyo imesheheni misitu, inayopatikana ndege wazuri wa angani. Wageni wanaotembelea hotelini hapo, huvutiwa na mandhari hiyo. Hoteli ya Matema ipo katika mwambao wa Ziwa Nyasa. Eneo hilo lilikuwa pori, lakini sasa limegeuka kuwa lulu kwa watu wa makabila tofauti ya ndani na nje ya nchi.

Eneo hilo limejaa utulivu na lina sauti za ndege. Baadhi ya wageni waliowahi kutembelea eneo hilo, wanadiriki kulifananisha na bustani ya Edeni. Kanisa la Uinjilisti lenye makao yake makuu Mbalizi, Mbeya Vijijini, ndicho chanzo cha kuwapo kwa hoteli hiyo, maarufu kama Matema Lake Shore Resort.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Kanisa hilo, Mchungaji Marcus Lrhner, anasema kuwa Kanisa la Uinjilisti lilifanya utafiti na kugundua kuwa eneo hilo linafaa kuweka vivutio na vivutio hivyo vinaweza kukuza sekta ya utalii nchini. Anasema kumekuwa na mafanikio kutokana na kuwapo kwa kivutio hicho.

Mafanikio hayo yanatokana na juhudi za kanisa hilo, kwa kupitia wafadhili wake, ambao kwa miaka nane sasa wamekuwa wakijitahidi kutunza mazingira. Mchungaji Lehner anasema kwamba utafiti uliofanywa pia ulizingatia kuwapo kwa eneo zuri la kuogelea, lenye mchanga safi na mzuri. Anasema Lake Shore Resort inatoa huduma za kulala na chakula cha asili, kinachoandaliwa kwa muda maalumu (kwa oda).

Pia, ina nyumba mbalimbali zenye jumla ya vyumba 22, ikiwamo vyumba vya kujihudumia (self contained) na vyumba vya vitanda viwili hadi vitano. Zipo pia nyumba za ghorofa, zinazomwezesha mgeni kutazama vizuri ziwa, lilivyo na umbo lake, kabla ya kutumia usafiri wa boti, wa miguu au gari. Huduma hizo pia hupatikana hapo.

Matema ipo katika eneo la Kaskazini, mwishoni mwa Ziwa Nyasa, ndani ya Wilaya ya Kyela. Ziwa lina upana wa wastani kilomita 60 na urefu wastani kilomita 550. Lipo kwenye Bonde la Ufa katika Afrika Mashariki na lina ujazo wa mita 500 kutoka usawa wa bahari. Ufukwe wa Matema unapambwa na safu za mlima Livingstone, wenye urefu wa mita 3,000.

Dk Salim: Ukiona nchi ina matatizo, wa kulaumiwa ni viongozi

Hawra Shamte


Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) Dk Salim Ahmed Salim ambaye ameeleza kuwa nchi inapokuwa na migogoro mingi wanaostahili kulaumiwa ni viongozi.


JITIHADA mbalimbali zinafanyika kuhakikisha kuwa nchi za Kiafrika zinafuata utawala wa sheria na pia kuzingatia haki za binadamu.

Mbali na nhi wahisani, nchi zilizoendelea na hata mashirika ya umoja wa mataifa kusisitiza umuhimu wa utawala wa sheria na haki za binadamu, zipo taasisi huru zilizo ndani ya nchi za Kiafrika ambazo nazo zinashajiisha uwepo wa utawala bora katika nchi za Afrika.

Mojawapo ya asasi za namna hiyo ni taasisi ya Mo Ibrahim ambayo mwanzilishi wake ni Dk Mohamed Ibrahim mzaliwa wa Sudan na tajiri aliyejikita katika masuala ya mawasiliano.

Mjumbe wa bodi ya taasisi ya Mo Ibrahim, Dk Salim Ahmed Salim anasema tatizo la nchi nyingi za Afrika ni ukosefu wa Utawala Bora, katika Makala hii, Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) Dk Salim aliyezungumza na mwandishi wetu HAWRA SHAMTE anaeleza jinsi ukosefu wa utawala bora unavyokinza demokrasia barani Afrika...

Swali: Bara la Afrika linakabiliwa na matatizo mengi ya kivita, ya kiuchumi, ya kisiasa na ya kijamii.

Mwasisi wa taasisi ya Mo Ibrahim, Dk Mohamed Ibrahim, raia wa Sudan hivi karibuni alizungumza katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam na kusema kwamba tatizo kubwa la nchi za Kiafrika ni ukosefu wa utawala bora, lakini dhana ya utawala bora ni pana sana, je, wewe unazungumza nini kuhusu dhana hii?

Jibu:Hakuna asiyetambua kuwa Bara hili lina nyenzo nyingi sana, lina kila aina ya mali, rasilimali yetu kubwa kuliko zote ni watu wetu ambao wanafanyakazi usiku na mchana tena katika mazingira magumu.

Kuna kila aina ya madini katika bara letu, dhahabu almasi na kadhalika, pamoja na hayo tuna mafuta pia katika bara letu. Kuna ardhi kubwa sana katika Afrika, kuna mito na maziwa ya kila aina lakini bado nchi zetu, watu wetu ndio wenye umasikini kuliko watu wote duniani.

Kwanini inakuwa hivyo? Kwa kweli hii inatokana na uongozi, kwa hiyo suala la uongozi bora ni suala la msingi, pale ambapo uongozi wa nchi umekuwa na uwezo wa kuhakikisha kwamba wanashughulikia maslahi ya watu wao, kunakuwa na tofauti kubwa.

Katika utoaji zawadi kwa viongozi bora, mchakato unaofanywa na taasisi ya Mo Ibrahim tunaangalia kiongozi alifanya nini kuboresha hali ya watu wake wakati akiwa madarakani.

Bara letu lina matatizo ya kiuchumi, lina matatizo ya rushwa kubwa sana, lina matatizo ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, lina matatizo ya uvunjaji wa haki za binadamu.

Taasisi ya Mo Ibrahim inachofanya ni kusaidia mchakato wa kidemokrasia na utawala bora, kwani si kweli kama bara la Afrika ni matatizo tu, si kweli kwamba kila nchi ya Afrika inanuka rushwa.

Kwa kweli kuna juhudi kubwa zinafanyika katika bara letu na mchakato wa kidemokrasia umepiga hatua nzuri pamoja na kwamba mwaka jana na mwaka huu tumepata misukosuko kidogo; matukio ya Guinea kwa mfano ambako wananchi wanauliwa na utawala wa kijeshi, matukio ya Mauritania, matukio ya Guinea Bissau na halafu zaidi matukio ya Somali na matukio ya Sudan.

Kwa mfano Sudan siyo suala la Darfur tu lakini ni nini mustakabali wa Sudan na nini itakuwa taathira ya mambo yanayotokea Sudan kwa bara letu la Afrika.

Kote unapoona kunakuwa na matatizo, kwa kweli wa kulaumiwa kwanza ni uongozi. Pale panapokuwa na uongozi safi, unaojitolea, uongozi usioshiriki ufisadi, uongozi unaojali zaidi maslahi ya watu wake, gurudumu la maendeleo linasonga mbele, lakini pale ambapo viongozi wanajilimbikizia mapesa, wanafanya mambo ya kidikteta na kadhalika, nchi hiyo hata ikiwa na nyenzo vipi haiwezi kwenda mbele.

Swali: Umeeleza kuwa katika maeneo yenye matatizo kama vile ya kivita ni ukosefu wa uongozi, lakini je, nchi kama Somalia ambayo wanapigana wenyewe kwa wenyewe na mpaka sasa inaitwa nchi isiyokuwa na dola je, tatizo ni hilo tu la kukosa uongozi bora?

Jibu:Ukitazama sana matatizo ya Somalia utaona kuwa ni ukosefu wa uongozi. Wanaopigana Somalia hivi sasa ni watu na wanaopata matatizo makubwa ni wananchi wa kawaida. Majemedari wa kivita ni viongozi mbalimbali wa Somalia na hawa walichofanya ni kuweka maslahi yao mbele kuliko maslahi ya watu wao.

Kama kuna nchi ya Kiafrika ambayo haikutegemewa kuwa na matatizo kama haya ilikuwa ni Somalia kwa sababu ni nchi ambayo watu wake wana dini, moja, wana utamaduni mmoja na wanazungumza lugha moja, isingetegemewa kuwa watu kama hao itatokea siku watapigana wenyewe kwa wenyewe, familia moja inaua familia nyingine.

Tatizo la Somalia ni ukosefu wa uongozi bora unaofikiria maslahi ya watu wake, lakini tatizo hilo si la Somalia tu, tazama Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) ni nchi moja ambayo pakiwa na utulivu, pakiendeshwa utawala bora itakuwa ni chachu ya maendeleo siyo ya Kongo tu bali ya sehemu kubwa sana ya bara la Afrika.

Lakini Kongo haikupata amani kwa muda mrefu sana, ingawa hivi sasa Rais Kabila anajitahidi kujaribu kuleta amani kwa kiwango kikubwa lakini bado kuna vita vya wenyewe kwa wenyewe, bado kuna watu wanafikiria maslahi yao, namna gani ya kupata fedha kwa njia za haramu kuwa ni jambo kubwa zaidi kuliko jambo jengine.

Swali: Unafikiri ni nini suluhisho la matatizo haya?

Jibu: Sidhani kama unaweza kuwa na suluhisho la namna moja kwa sababu kila pahala na mazingira yake.

Chukulia Somalia kwa mfano, Somalia kuna Al Shabab, hawa wanasema wao ndio Waislam safi na wanataka kuleta Uislam, lakini ni upuuzi mtupu, kwa sababu haiwezekani kuwa brandi yako tu ya Uislam ndiyo iwe bora kuliko nyingine hufiki mbali.

Lakini pia Somalia ilipuuzwa, baada ya matatizo yaliyotokea Mogadishu wakati wa Jenerali Aideed na Marekani kupata msukosuko; wanajeshi wa Kimarekani waliingia kwa dhamira ya kutoa misaada ya kibinadamu 'humanitarian' halafu humanitarian ikabadilika wakaanza kuingia katika mapambano, askari wa Kimarekani wakauliwa katika helikopta yao na wakaburutwa; toka wakati ule Marekani iliitenga kabisa Somalia.

Nakumbuka nilipokuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Afrika, nikienda Marekani naweza kuzungumza tatizo lolote lakini si Somalia, ilikuwa ukitaja Somalia wanakwambia achana nao hao.

Kwa hivyo ni nchi ambayo ilitengwa, Marekani waliitenga lakini na jamii kubwa pia waliitenga, tukaiachia inaendelea tu…

Jingine ni kuwa viongozi wa nchi ile wakaanza kugawana; Somalia iliyokuwa jamii moja, wakaanza kugawana sasa kuna makabila, ukoo, familia na kadhalika. Ingawa hivi sasa Somalia kuna juhudi zinafanyika lakini juhudi zozote zinazofanyika lazima waishirikishe Al Shabab. Huwezi kupata ufumbuzi wa kivita pale lazima pawe na mazungumzo ya dhati kabisa…

Kwa DRC juhudi kubwa imefanyika, hali iliyoko DRC sasa hivi tofauti sana na miaka mitatu, minne, mitano iliyopita lakini bado kuna matatizo Mashariki ya Kongo, kwanini? Moja ya matatizo yetu katika bara letu, imekuwa hizi rasilimali tulizonazo, nyenzo tulizonazo, madini tuliyonayo baada ya kuwa faida kwa watu wetu imekuwa kama ni dhambi, kama ni laana, sasa inakuwa pale palipo na mafuta matatizo, palipo almasi matatizo, palipo dhahabu matatizo, mimi nadhani changamoto kubwa ya bara letu ni namna gani ya kugeuza hizi rasilimali, hizi nyenzo tulizonazo, baada ya kuwa ni sehemu ya matatizo iwe ni sehemu ya kuleta maendeleo kwa bara zima na kwa manufaa ya watu wetu.

Kwa upande wa Sudan kwanza tatizo lilikuwa baina ya Kaskazini na Kusini, vita viliendelea kwa muda mrefu sana na watu wengi walifariki, takwimu zinasema watu kama milioni nne walifariki katika vita vya wenyewe kwa wenyewe baina ya Kaskazini mwa Sudan na Kusini mwa Sudan.

Mwaka pale. Mwaka 2005 yakapatikana makubaliano ya kijumla (Comprehensive agreement).

Halafu kuna suala la Darfur, huko nako kuna matatizo makubwa, mpaka hivi sasa juhudi zilizofanyika kujaribu kutanzua hazijafanikiwa.

Lakini hivi sasa hali ya Sudan imekuwa ngumu zaidi na mimi binafsi inanitisha kidogo, inanitisha kwa sababu siyo tu suala la Darfur lakini kuna uwezekano wa kuwa na fujo zaidi kama ndugu zetu wa serikali ya Sudan ya Kaskazini na ndugu zetu wa SPLM hawakuwa na makubaliano ili kura ya maoni ya mwaka 2011 ikafanyika katika mazingira mazuri na halafu wakaheshimu matokeo ya kura ile.

Tatizo lililopo hivi sasa inaonyesha kuwa badala ya kuwa na umoja wa Sudan kuna uwezekano kuwa watu wengine wakataka kujitenga.

Najua kama kuna watu wengine wanafurahia kujitenga, wanasema kujitenga ni nzuri, lakini ukianza suala la kujitenga katika bara letu na hasa katika nchi kubwa kama Sudan kuna taathira zinazoweza kutokea siyo tu ndani ya Sudan lakini pia katika majirani wa Sudan.

Kwa hiyo mimi nafikiri hili jambo la Sudan kwa sasa Jumuiya ya Kimataifa na hasa nchi za Kiafrika zinapaswa kulipa uzito wake na kujaribu kuhakikisha kwamba katika huu muda uliobakia kila jitihada zinafanywa ili kuwafanya wananchi wa Sudan wajione kuwa ni wamoja na hasa ambao wanahisi kwamba wameonewa.

Tatizo kubwa la Sudan ni kwamba wananchi walio katika pembezoni wanahisi kwamba wametengwa (siyo kama hawana sababu) na maslahi yote na maendeleo yote yanatokea katika sehemu moja tu ya Sudan.

Jambo moja ambalo linaweza kuwa zuri ni kujaribu kuibana serikali ya Sudan kuzungumza na ndugu zetu wa SPLM waandae mazingira ili wananchi wa Kusini mwa Sudan watakaopiga kura waseme kwamba jamani tuhakikishe hili suala la umoja linapatikana.

Lakini kama hilo halipatikani basi angalau waandae mazingira ya kuwa huo mchakato wa kura za maoni uwe wa amani na wakubaliane na mapema kama kuna kura ya maoni likitokea hili tutafanya nini, lisiachwe tu kama bomu likapasuka kwa sababu kama hakuna hivyo kuna hatari kabisa kwamba ufikapo mwaka 2011 bila mawasiliano,

bila mapatano bila ushirikiano hali ya Sudan ikaendelea kuwa tete na inapoendelea kuwa tete haitokuwa tu Kusini mwa Sudan lakini itaathiri pia sehemu mbalimbali za Sudan ambazo pia zina matatizo yake, Darfur, Kordufan, Blue Nile na kadhalika.

Swali: Kumezuka mtindo mwengine wa demokrasia barani Afrika, sasa hivi demokrasia mbali ya kuwa ni mchakato wa uchaguzi lakini mwisho wa siku inabidi lazima watu wakae katika meza za majadiliano. Na zimezuka hizi serikali za mseto kama Kenya na Zimbabwe, je, nini maoni yako kuhusu hilo?

Jibu: Kila sehemu ina mazingira yake maalum. Demokrasia maana yake ni kwamba wananchi wenyewe wawezeshwe kuchagua viongozi wao na namna serikali wanayoihitaji na serikali hiyo iwaongoze kwa muda gani na wawe na uwezo wa kubadilisha viongozi wao muda ule unapofika.

Lakini mazingira yatofautiana, kwa mfano; katika Kenya baada ya mauaji yaliyotokea mara baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 na kuleta taathira kubwa kwa maendeleo ya Kenya kulikuwa na umuhimu wa kutafuta usuluhishi na mawasiliano na maafikiano ya namna fulani, kwa hivyo serikali ya mseto iliyoundwa Kenya, ilikuwa na madhumuni hayo.

Ukitazama mazingira yalivyokuwa, ukawa mkaidi tu ukasema hakuna haja ya kuwa na serikali ya pamoja kwa kweli unakosea, unawatakia ndugu zetu wa Kenya waendelee katika maafa tu.

Zimbabwe kidogo tofauti na Kenya, lakini kama wenyewe wamekubaliana, tunapaswa kuheshimu makubaliano. Ukitazama uchaguzi wa Zimbabwe ulivyokwenda, Chama cha MDC katika uchaguzi wa wabunge kilishinda, suala lilikuwa je, uchaguzi wa Rais ulikuwaje? Bahati mbaya mazingira hayakuwa yanaruhusu kufanya uchaguzi ambao ungekuwa huru na wa haki.

Kwa hivyo katika mazingira kama hayo, mimi nadhani ilikuwa ni busara kujaribu kuwakutanisha viongozi ili waweze kuona jinsi ya kuwa na muundo wa serikali ambao utazingatia maslahi ya watu wote wa Zimbabwe.

Na pamoja na kuwa bado kuna matatizo nchini Zimbabwe, lakini nadhani hilo lilikuwa ni jambo la busara. Mimi nadhani pale ambapo kuna ushindani mkubwa sana wa kisiasa na ambapo bado watu hawajaweza kustahmiliana na kuweza kujua kuwa wewe unaweza ukawa chama fulani, mimi nikawa katika chama kingine, hata katika familia moja; baba akawa chama fulani, mama akawa chama kingine na watoto wakawa chama kingine na mkaendelea katika familia bila matatizo; pale ambapo ustahmilivu kama huo haupo.

Ni muhimu sana kufanya utaratibu wa kushirikisha watu wote katika utawala, vinginevyo utaendelea katika mapambano tu na panapo mapambano ni muhali kupata maendeleo ya kudumu ya kiuchumi.

Jamani hatupungi mashetani hapa, tunasoma

Na Brandy Nelson, Chunya




Wanafunzi wakiwa darasani wakiendelea na masomo


HADI kufikia mwaka 2000 kijiji cha Udinde kilikuwa na shule moja ya msingi iitwayo Udinde iliyochukua watoto kutoka vitongoji vya jirani pia, lakini ulipoanzishwa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (Mmem) mwaka 2002 ilionekana haja ya kufanya maboresho.

Shule hiyo ilipachuliwa ikazaa shule nyingine ya msingi katika kitongoji cha Iboma mwaka 2003.

Uamuzi wa kujenga shule nyingine, mbali ya kufanya maboresho ulilenga pia kuwapunguzia wanafunzi adha ya kutembea umbali wa kilomita 10.

Serikali ya kijiji hicho kilichopo kata ya Kapalala tarafa ya Kwimba wilaya ya Chunya mkoani Mbeya ikitumia pesa zilizotokana na Mmem ilifanikiwa kujenga darasa moja tu na hadi sasa halijakamilika wala halijaongezwa darasa jingine wala vyoo na nyumba za mwalimu.

â€Å“Shule hii ilimegwa kutoka shule ya msingi Udinde ambapo hapa Iboma tuliletwa walimu watatu na mazingira yenyewe ni kama haya unavyoyaona. Wazazi walichangia kujenga darasa hili moja na serikali kupitia Mmem ikamalizia paa ingawa darasa lenyewe bado halina sifa ya kuwa darasa kwani halijakamilika,” anasema mwalimu Albert Juakali ambaye alikutwa akifundisha hisabati wanafunzi wa darasa la kwanza.

Uamuzi wa haraka uliofanywa na walimu ni kuhamishia ‘mikoba’ yao kwenye mti wa mbuyu ulio jirani na kuweka mbao. Upande mmoja wanakaa darasa la kwanza, halafu upande mwingine darasa la pili, la tatu, la nne, la tano nk. Wakati wa juakali shida na wakati wa mvua ni likizo.

Mwenye masikitiko zaidi ni mwalimu mkuu wa shule, Onesmo Mdamu ambaye anasema;"Sikiliza, shule hii ina muda wa miaka sita mpaka sasa lakini ina darasa hili moja tu na ambalo linatumika kwa ajili ya watoto wa darasa la sita na hawa wa madarasa mengine wanasoma kwenye mti wa mbuyu ambao pale kuna madarasa matano yaani la kwanza, pili, tatu, nne na tano kama mnavyoona wenyewe."

Hayo ndiyo maisha ya wanafunzi wa shule hiyo na uamuzi wa kutumia mti huo kama darasa ulipitishwa na kamati ya shule.

Madhara

Mazingira hayo yamewasaidia zaidi watoto wasiopenda elimu maana huona heri kwenda kujishughulisha na uvuvi wa samaki kwenye Ziwa Rukwa lililojirani na shule hiyo badala ya kushinda kwenye juakali chini ya mti.

"Mazingira ya shule hii ni magumu kutokana na kuwa na darasa moja ambalo linatumiwa na wanafunzi wa darasa la sita. Shule yenyewe kama unavyoiona iko kandokando ya Ziwa Rukwa hivyo inapelekea watoto kuamua kujishughulisha na ajira ya uvuvi wa samaki kutokana na mazingira magumu ya shule na ugumu wa maisha wa familia zao na hivyo kukosa haki ya kupata elimu bora," anaongeza Juakali.

Aliyeamua kubadili matumizi ya mbuyu kutoka kwenye imani za asili kwamba ni makazi ya mashetani hadi kuwa darasa la wanafunzi 134 ni kamati ya shule. Kamati hiyo ya shule imeshindwa kuhamasisha wananchi yajengwe madarasa mengine.

Kinachofanyika chini ya mti wa mbuyu, Mdamu anasema wanafunzi huchukua mabanzi na kuweka juu ya matofali na sehemu ya kuandikia wakitumia matofali kama meza na wengine wakishindwa kupata mabanzi hutumia matofali kama viti.

"Hali hii ni mbaya kielimu kwani hata sisi walimu hatujui tumwachie nani hawa wanafunzi, basi tumeona tuungane na usemi usemao 'Ualimu ni Wito', lakini kwa ujumla hali ni mbaya sana. Hata mahudhurio ya wanafunzi ni finyu kutokana na kukatishwa tamaa na mazingira na kupelekea kujiingiza katika shughuli za uvuvi wa samaki,” anasema

Mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo, Leopard Ngairo mbali ya kuelezea historia anakiri kwamba mazingira ya ufundishaji ni magumu na yanachangia wanafunzi kukosa elimu bora na hivyo wengine kuamua kuacha shule na kujiingiza katika ajira ya shughuli za uvuvi wa samaki.

"Shule ina darasa moja pekee, ina uhaba wa madawati, ofisi za walimu, vifaa vya kufundishia hakuna ambapo kwa sasa shule ina vitabu viwili kwa kila darasa, kwa kweli walimu wanashindwa kutoa elimu ipasavyo kwa wanafunzi," anasema Ngairo.

â€Å“Hii shule ina matatizo makubwa huwezi kufananaisha na shule zingine kwani wazazi wengi wanakatishwa tamaa na mazingira yake na inasababisha wazazi kuwaruhusu watoto wao kutafuta ajira katika shughuli za uvuvi badala ya kwenda shule,” anasema

Darasa la saba

Septemba mwaka huu walimu na kamati ya shule walisugua vichwa kuona namna nzuri ya kuwasaidia wanafunzi wa darasa la saba waliotarajiwa kufanya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi. Hapo tena, walimu na kamati ya shule walikubaliana kulihamishia darasa hilo Udinde kwa ajili ya kumalizia elimu yao ya msingi.

"Hapa kwa kweli hakuna elimu bora inayopatikana kwani mazingira yote kwa ujumla ni magumu siyo kwa wanafunzi wala sisi walimu kwani hakuna hata vitendea kazi na tunaishi mbali na shule na inatulazimu kutembea umbali wa kilometa tisa ili kuweza kufika hapa shuleni," anasema Mdamu.

Mahitaji ya shule hiyo ni kuwa na walimu watano lakini waliopo wanaofanya kazi ni wawili pekee, hakuna vitabu vya kufundishia kwani vilivyopo ni vitabu viwili kila darasa na kwamba madawati ni tatizo kubwa hali inayopelekea watoto hao kukaa kwenye matofali.

Walimu hao wamekuwa wakifundisha kwa moyo wote na wamekuwa wakipeleka ripoti kila mwezi kwa afisa elimu wa halmashauri kuwajulisha hali halisi ya shule, lakini hakuna kinachofanyika na kuifanya shule hiyo kutokuwa na maendeleo yoyote.

Mdamu analalamika pia kwamba hali hiyo kwa kiasi fulani inachangiwa na baadhi ya wazazi katika kitongoji hicho kukosa mwamko wa kuwapeleka watoto wao shule na badala yake wamekuwa wakijikita zaidi kwenye shughuli za uvuvi kuliko suala la elimu kutokana na mazingira ya shule hiyo.

Mwalimu mkuu anadhani kwamba ufumbuzi wa haraka juu ya matatizo ya shule umo kwenye mikono ya viongozi wa wilaya na mkoa.

"Kama viongozi wa serikali ya wilaya na mkoa wangetembelea na kushuhudia mazingira ya shule na kuwahamasisha wananchi wajitolee nguvu zao kujenga shule ni jambo ambalo lingesaidia watoto hao kupata elimu bora badala ya bora elimu ambayo wanaipata kwa sasa," anasema.

Wanafunzi nao wamefikia hatua ya kuuona ukweli kwamba hakuna wanachopata katika mazingira kama haya. Adela Alex, mwanafunzi wa darasa la sita anasema mazingira ya shule hiyo ni magumu na hivyo kupelekea kushindwa kupata elimu bora na kusabibasha baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo kukatamaa na kuendelea na shule na kujiingiza katika shughuli za uvuvi wa samaki kwa kufanya vibarua na kujipatia fedha kidogo.

"Kwa kweli sisi wanafunzi tunaona hali hii ni mbaya kwetu tunaona kama tumetengwa labda sisi siyo raia wa Tanzania au labda serikali inatuona kama wanyama, haiwezekani tukawa tunasoma shule katika mazingira haya ya chini ya mti wa mbuyu halafu tukasema kuna kitu tunakipata; hakuna tunachokipata hapa chini ya mti,"anasema kiongozi wa wanafunzi Emanuel Mkombe.

Anasema kuwa mazingira hayo hayawawezeshi kusoma vizuri yanawakatisha tama ndiyo maana kuna baadhi ya wanafunzi wamekimbia na kuamua kufanyakazi ya vibarua ziwani. Lakini kuna wanafunzi wengine ambao wana nia ya kusoma ndiyo maana wameendelea kuwa wavumilivu na kukubali kusoma chini ya mti wa mbuyu.

Mkombe anasema kuwa kuna hatari ya wanafunzi wote wasichana kwa wanaume kukimbilia ziwani kwa ajili ya kupata ajira katika shughuli za uvuvi ambako wanalipwa fedha kidogo kuanzia kati ya Sh 500 hadi Sh 200 kwa kazi wanazopewa ikiwa ni pamoja na kupasua samaki, kutafuta kuni, kuosha nyavu na kukausha samaki.

Anasema kuwa ajira hiyo ni mbaya kwa watoto na ni hatari kutokana na wengi wao kupata ajali mbalimbali ziwani ikiwa ni pamoja na kukamatwa na mamba na kupoteza maisha bado wakiwa na umri mdogo.

"Tunaiomba Serikali iliangalie suala hili la mazingira ya shule yetu ili na sisi tuweze kupata haki ya kupata elimu kama wanavyopata wenzetu ili tuweze kuokoa maisha yetu na kujinusuru na ajira hii mbaya ya watoto katika Ziwa Rukwa kwani sidhani kama kuna watoto wenzetu wengine wanasoma katika mazingira kama haya," anasema.

Mtazamo huo ndio alionao Ngairo kwamba: "Kama unavyoona tunaendelea kuomba wananchi na wadau wa Elimu kutuchangia ujenzi wa shule yetu na na sasa tumeanza kujenga darasa lingine na nyumba za Walimu kwa mchango wa nguvu za wananchi lakini bado tunahitaji msaada mkubwa kutoka kwa wananchi,wadau wa elimu na Serikalini."

Katibu wa Elimu, Uchumi, Malezi na mazingira wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Chunya, Philipo Mulugo anasema mazingira ya Iboma yanatia uchungu.

"Mazingira ya shule ya Iboma yanatia uchungu sana kwani serikali kupitia ilani ya CCM inapaswa kuliangalia hili na sisi kama viongozi wa chama na wadau wa elimu tunatakiwa kulipokea kwa masikitiko ikiwa ni pamoja na kushiriki kwa kuisaidia serikali katika ujenzi wa shule hii ya Iboma," anasema

"Sidhani kama kuna mtu ambaye atasikia taarifa ya mazingira ya shule ya Iboma ataamua kukaa kimya, basi huyo atakuwa siyo mpenda maendeleo ya elimu na mimi nitakwenda huko kama katibu wa elimu na nitapeleka mifuko ya saruji 10 ili iweze kuwasaidia,"anasema

Mulugo ametoa wito kwa wanachi wa Iboma na wale wa kata ya Kapalala wanaoishi nje kujitoa kwa hali na mali ili kuisaidia shule hiyo kuwanusuru wanafunzi kusoma chini ya mbuyu ili waweze kupata elimu bora.

Lakini Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Chunya Maurus Sapanjo amesema kuwa haifahamu hiyo shule na hajawahi kufika katika shule hiyo.

"Kwa kweli lazima niwe mkweli na muwazi siifahamu hiyo shule na wala afisa elimu wangu hajawahi kunipa taarifa ya shule hiyo kwamba kuna shule ina darasa moja na wanafunzi wanasoma chini ya mti wa mbuyu. Ndiyo kwanza nimeisikia kupitia gazeti la Mwananchi na imenisikitisha sana kuona katika wilaya yangu kuna shule yenye matatizo kama haya,"anasema.

Sapanjo anasema kuwa siyo nia yake na hajafurahishwa na taarifa hizo kwani malengo yake ni kuhakikisha baada ya miaka 10 watoto wa wilaya ya Chunya wanafika vyuo vikuu.

Anasema angekuwa anaijua shule hiyo asingekimbilia kujenga shule za sekondari za kata 18 wakati kuna shule ya msingi ina darasa moja na wanafunzi wanasomea chini ya mti wa mbuyu.

"Nimemwagiza afisa elimu wangu pamoja idara nzima ya elimu kuhamia shuleni hapo na kuhakikisha madarasa yanajengwa kwa haraka ili kuondokana na adha hiyo," anasema juu ya hatua alizochukua.

Kuhusu wanafunzi kujishughulisha na uvuvi wa samaki badala ya masomo, amesema msako mkali unafanyika kuhakikisha watoto wote wanarudi shuleni haraka na kuwachukulia hatua za kisheria wazazi wote watakaobainika wanashiriki katika kuwaruhusu watoto wao kufanya kazi ya vibarua ya uvuvi wa samaki na shughuli nyingine ziwani.

Mtikisiko wazuka Baraza la Mawaziri

Mwandishi Wetu
Raia Mwema

Novemba 25, 2009

  • Kikwete yaanza kumshinda
  • Sasa hata Dk. Shein azoza

SIKU chache tu baada ya kutuma ujumbe kwamba akipita mwakani hatabeba mawaziri wazee, Rais Jakaya Kikwete ameanza kutekeleza azma hiyo kwa kuwatangazia mawaziri wake kwamba amechoshwa nao kwa kuwa hawamsaidii, imefahamika.

Habari ambazo Raia Mwema imepata zinasema kwamba Rais Kikwete na hata wasaidizi wake, Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wamekuwa wakali isivyo kawaida yao katika vikao vyao vya kazi.

Kwa mujibu wa habari hizo, katika kipindi kiasi cha wiki mbili zilizopita, Rais Kikwete amekutana na mawaziri wake mara mbili na katika vikao hivyo amesema waziwazi kwamba mawaziri wake hawamsaidii kama alivyotarajia wakati akiwateua.

"Hakikua kikao cha baraza, lakini alizungumza kwa ukali akiwaambia kwamba alipowateua alikuwa na matumaini makubwa nao kwamba atakuwa amepunguza kwa kiasi kikubwa uzito wa kazi.

"Akawaambia amekuwa akilazimika kufanya mambo mengi ambayo yangeweza kufanywa na mawaziri wake aliowaamini na akawapa dhamana," anaeleza ofisa mmoja wa serikali aliyezungumza na Raia Mwema wiki kwa masharti ya kutotajwa gazetini.

Mtoa habari huyo amesema wiki iliyopita Rais Kikwete alikuwa mkali kwa wasaidizi wake kuliko ilivyopata kutokea tangu aingie madarakani mwishoni mwa mwaka 2005.

Imefahamika kwamba kabla ya kikao cha wiki iliyopita, kilichofanyika nje ya Dar es Salaam, Rais Kikwete aliwaita mawaziri wake ghafla katika hatua ambayo ilizua hofu miongoni mwao wakiamini kwamba huenda alitaka kuvunja Baraza lake.

Habari zaidi zinasema katika kikao cha awali waziri mmoja mwanamke alikwepa kuhudhuria baada ya kupata fununu kwamba Rais Kikwete alikuwa amekerwa na baadhi ya kauli zake za hivi karibuni.

Habari zinaeleza kwamba, hata Dk. Shein ambaye anafahamika ya kuwa mara nyingi hana hulka ya ukali amebadilika, na sasa naye ameanza kuwa mkali waziwazi katika vikao vya utendaji.

"Kuna kikao kimoja ambacho baada ya Rais kumbana waziri mmoja kutokana na kuwasilisha waraka uliokuwa umejaa mapungufu, Makamu naye alizungumza kwa ukali akimtaka waziri huyo kuacha kufanya mambo bila kufuata taratibu," anasema mtoa habari huyo.
















Rais Jakaya M. Kikwete

Anaongeza: " Katika kikao hicho Rais alimkatiza waziri huyo mara kwa mara akitaka ufafanuzi na wakati mwingine kumlazimisha waziri huyo kubadili baadhi ya mambo ambayo aliona yana makosa mengi katika waraka wake.”

Ukali wa ghafla wa Rais Kikwete, Dk. Shein na Pinda unatajwa kuwa umechochewa na utendaji usioridhisha wa mawaziri wengi unaosababisha viongozi hao wa juu kabisa kulazimika kufanya kazi ya ziada.

Katikati ya habari hizo ni hali kwamba mawaziri wengi wanashindwa kuitetea na kuisimamia Serikali ndani na nje ya Bunge, mbele ya umma na katika shutuma nyingi zinazotajwa kwenye vyombo vya habari. Anasema mtoa habari huyo: "Rais alieleza wazi kwamba anakerwa na taarifa za mara kwa mara katika vyombo vya habari zikionyesha udhaifu mkubwa wa Serikali yake huku wasaidizi wake wakiwamo mawaziri wakishindwa kutoa hoja zenye nguvu au mkakati mahususi wa kukabiliana na taarifa hizo.”

Japo tathmini inaonyesha kwamba si rahisi katika muda mfupi uliobaki kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu kuwa na mabadiliko katika Baraza la Mawaziri, Raia Mwema imearifiwa ya kuwa tayari mchakato umeanza ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa wa kuchunguza mienendo ya watu wakiwemo wajumbe wa sasa wa Baraza la Mawaziri na wajumbe watarajiwa ikibidi kufanyika kwa mabadiliko.

Habari zaidi zinaeleza kwamba yamekuwapo mapendekezo kwa Rais Kikwete ya kutaka abadili baadhi ya mawaziri waliopo kwa baadhi ya wabunge ambao wamekuwa wakitajwa kuwa wako msitari wa mbele katika inayotajwa kuwa ni vita ya ufisadi katika hatua ya kukisafisha Chama cha Mapinduzi (CCM) katika tuhuma za ufisadi na migawanyiko ya dhahiri ili kuvutia kura katika uchaguzi wa mwakani.

Mbali ya kuingiza sura mpya na kupunguza baadhi ya mawaziri, kuna taarifa kuwa yapo mapendekezo kwa Rais ya uwezekano wa kupandisha ngazi naibu mawaziri walioonyesha uwezo mkubwa.

Haya yakiendelea zimekuwapo taarifa za wizara mbalimbali ambako wafanyakazi wanawalalalimikia mawaziri wao kwa utendaji kazi usioridhisha.

Kati ya waliotajwa na wafanyakazi hao ni pamoja na Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, John Chiligati; Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na Naibu wake, Dk. Makongoro Mahanga; Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Sophia Simba.

Lakini akizungumza na Raia Mwema wiki iliyopita Chiligati alisema “hawezi kufanya mtihani na kujisahihishia mwenyewe.”

“Hayo maoni ya watu siwezi kuyaingilia, mimi siwezi kufanya mtihani na kujisahihisha mwenyewe lakini naamini watendaji ofisi wanajua naingia ofisini saa ngapi na natoka saa ngapi,” alisema Chiligati na alipoulizwa kuhusu shughuli za chama kuingilia majukumu ya serikali, alisisitiza kutotaka kujisahihishia mtihani.

Katikati ya mwezi huu akizungumza na vijana wa kutoka nchi mbalimbali za Afrika mjini Dar es Salaam, Rais Kikwete alituma salamu za mwanzo kwa wateule wake kwa kuwaambia vijana hao ya kuwa endapo atajaliwa kuongoza tena Tanzania mwakani, atafanya jitihada kubwa kuondokana na sura za wazee ambao atawabadilisha na vijana.

Akizungumza katika mkutano wa vijana hao wa kulea viongozi wa Afrika, Rais Kikwete alisema atafanya mabadiliko makubwa kwenye Serikali yake akshinda uchaguzi ujao.

Alisema Kikwete: “Wale viongozi wa rika langu, lazima waanze kuwaachia nafasi vijana. Tunahitaji wakuu wa wilaya vijana zaidi, wakuu wa mikoa vijana zaidi na hata mawaziri vijana zaidi. Ndivyo ilivyotokea kwetu sisi wakati tukiwa vijana.”

Mheshimiwa Rais Kikwete na first Lady wakitalii huko Jamaica


Rais Jakaya na mkewe Salma wakibembea hewani kutalii vivutio nchini Jamaica pamoja na Waziri wa Utalii nchini humo,Edmund Barlett (kulia) na Horace Clarke, mmiliki wa bembea hilo lipitalo meta 50 hewani umbali wa kilometa mbili.

Wednesday, November 25, 2009

Mabadiliko huja kwa dhamira ya kweli ya Kutekeleza Ahadi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jakaya Mrisho Kikwete.
Sijui kama kweli tunataka mabadiliko au tunaombea mabadiliko yatokee. Sijui kama tunafanya ili kusababisha mabadiliko au tunasubiri wengine wafanye ili tufurahie mabadiliko; Sijui hata kama tunajua vizuri ni mabadiliko gani hasa tunayataka na kama tunataka ni juhudi gani tumezifanya kushiriki kwenye mchakato wa kuleta mabadiliko hayo.


Tunaweza kubishana vijiweni na kwenye mitandao na kujaribu kubadilishana mawazo mchana kutwa na usiku kucha lakini mabadiliko hayaji kwa kusema. Mabadiliko hayaji kwa kupigiwa magoti au kwa kukemea giza usiku. Mabadiliko husababishwa na kutekelezwa.

Tukijifunza kwenye kampeni ya Obama utaona kuwa Wamarekani hawakuombea tu kuwa kiongozi mzuri au wamtakaye aje na alipojitokeza hawakukaa pembeni kuombea kuwa afanye vizuri ili hatimaye "alete mabadiliko" wanayoyataka. Wamarekani walishirikishwa katika kampeni kuanzia kuchangia fedha, muda wao, vipaji vyao n.k

Je kwanini tunafikiri sisi Tanzania tutapata mabadiliko kwa kubishana vijiweni na kwenye mitandao na kuoneshana nani anajua nini na anahusika na nini? Mabadiliko ndugu zangu hayaji kwa kunuia au kuwa "kusudio zuri" au kwa kujua ufisadi ulivyo mbaya na fisadi ni nani!!

Mabadiliko huletwa na watu waliokusudia kuleta mabadiliko hayo.

Je una mawazo yoyote kuhusu kushiriki katika mabadiliko tunayoyataka au kutoa mchango wa aina yoyote?

Niandikie utupe mawazo yako.

kyelacommunity@live.com

Huu si wakati wa Kukata tamaa



Mbunge wa Kyela Dk. Harrison Mwakyembe

Bila ya shaka mlolongo wa matukio kadha wa kadha yanaweza kumfanya mtu yeyote kushika tama na kukata tamaa. Hasa inapotokea matukio ambayo yanaihusu familia zetu, jamii zetu, au nchi yetu. Msururu wa kashfa ambazo zimeiandama nchi na viongozi wetu bila ya shaka vinaweza kukufanya ujisikie mpweke na mnyonge na zaidi kuweza kujiuliza "Tanzania ina matatizo gani?".

Kwa wengine kujiuliza swali hili kunaendana na hisia ya kuachwa peke (abandonment) na kukata tamaa (despair). Na zaidi ya yote kuna wengine ambao wanaweza kujihisi kuvunjwa moyo (discouraged) na hivyo kuona kuwa hakuna lolote na chochote kinachoweza kufanyika Tanzania ambacho kinaweza kuturudisha kwenye matumaini?

Je huu ndio wakati wa kukata tamaa na kuwaachia mafisadi wafanye wapendavyo? Je huu ndio wakati wa kukubali viongozi wabovu na wasio na uwezo alimradi tuendelee katika hali ya utulivu, amani na mshikamano? Je huu ni wakati wa kusalimu amri na kukubali kile ambacho kimetuangukia na kuwa yote ni "mapenzi ya Mungu"?

Je unajihisi kukata tamaa ukiangalia mambo yanayoendelea katika nchi yetu?

Niandikie:

Tabia za Watoto zinatokana na Makuzi.

Na Africar T Kagema




Makuzi ya mtoto yanaweza kugawanywa katika nyanja kadhaa mfano makuzi ya kimiwili, kiakili, kimaono,kimaadili n.k. Katika makala hii tutajaribu kuona jinzi marafiki wanavyoweza kuathri ukuaji wa mtoto kimaadili. Upo msemo kuwa tabia ya mtu inaweza kueleweka vyema kwa kuzingatia tabia ya rafiki yake au marafiki zake. Msemo huu unatilia mkazo dhana nzima ya kuchagua marafiki wema ili kujenga tabia njema.

Malezi ya mtoto huanzia nyumbani kwa wazazi wake. Kipindi cha awali cha maisha ya mtoto (miaka 0-2) mtoto huishi zaidi katika mazingira ya nyumbani na tabia zake zote hutegemea tabia za watu wa nyumba husika. Baada ya hapo mtoto huanza kutoka na kuchanganyika na watoto wa nyumba jirani pamoja na watu wa vimo tofauti na yake.

Pia kwa hali ilivyo sasa watoto huanza kwenda shule za awali au madrasa (miaka 3-6). Baadaye hujiunga na shule za msingi kuanzia miaka 7 - 14 na hatimaye kuingia sekondari akiwa na umri wa miaka 15-19. Tutaona kuwa umahiri wa stadi mbalimbali kama lugha, michezo,hobi na mengineyo hupatikana katika kipindi ambacho mtoto ameshaanza kuwa na maingiliano na watu wa nje ya familia yake.

Tutakubaliana kuwa wazazi kama waalimu wa mwanzo kabisa wa motto (Nursery Teachers) watahusika sana na mustakabali mzima wa tabia za mtoto wako. Hawa ndiyo wenye jukumu ya kumjengea msingi mzuri wa maadili ya jamii ambapo chimbuko la tabia njema hupimwa kutokana na jinsi mtu anavyoweza kutenda mambo yake kwa kuzingatia maadili ya jamii husika.

Katika nyumba ambayo maadili huchungwa watoto hujifunza pia kuchunga maadili. Marafiki katika familia hizi hulingana kabisa na familia husika katika suala zima la kuzingatia maadili.

Utakapofika wakati wa mtoto kutoka nyumbani na kuingia mitaani tayari kuwa amejengewa msingi ambao utamsaidia kupata marafiki wema. Awali wazazi humsaidia mtoto kuchagua marafiki ambao huwa ni wale wanaotoka katika familia zenye maadili mema.

Msingi huu pia humsaidia mtoto kuchagua hobi nzuri ambazo haziendi kinyume na maadili ya jamii. Izingatiwe kuwa tabia za wizi, uvutaji wa bangi, madawa ya kulevya, utoro shuleni n.k. huigwa na watoto wakiwa katika vikundi. Kama wazazi watawaacha watoto wao bila kuwapa muongozo bora wa namna ya kupata marafiki wema basi wasishangae watoto wao kukosa kabisa makuzi mema katika hii nyanja ya maadili na hivyo kuishia kuwa watu mizigo "liability" katika jamii.

Hivyo natoa wito kwa wazazi kukaa na watoto wao bila kuchoka kung’amua mabadiliko ya tabia zao ili waweze kuzibadilisha mapema kabla hazijazoeleka na kuonekana ni kitu cha kawaida kwao. Ni vema pia kufuatilia mafundisho wanayopewa watoto wawapo shule za awali ili kutambua maadili yanayoizunguka shule hiyo na kuchukua hatua mapema.

Kanisa au Misikiti ni sehemu muhimu sana kwa watoto kuhamasishwa kuhudhuria ili waweze kujifunza maadili ya Mungu. Watoto wanaoshindwa kuhudhuria makanisani au Misikitini huwa wanakosa mengi kwani zile ni sehemu zinazofundisha watoto maadili mema katika jamii. Vipindi kama vya Sunday School kwa wakristo na madrassa kwa waislam ni vipindi vizuri sana katika maadili ya watoto katika umri wao mdogo.

Watoto wakalishwe chini na waelezwe kipi cha kufanya na wakati gani, na kipi cha kutofanya na katika mazingira gabi. Wazazi wasipuuzie na kuacha tabia mbaya za watoto zikiendelea kukomaa, kwani kwa kufanya hivyo kutasababisha kushindwa kuwarekebisha mara wakiachwa na tabia zao. Kama wazee wasemavyo ‘’mkunje samaki angali mbichi’’, kwani akikauka (akikomaa awezi kufunzika tena).

Watoto wadogo wanahitaji watu wazima ili waweze kuwaongoza na kuwasaidia ili wajifunze tabia na maadili yanayokubalika na yale yasiyokubalika. Wanahitaji pia watu wa kuwasaidia ili wajifunze namna ya kushirikiana na wengine. Jinsi tunavyotoa muongozo wa namna hii inategemea malengo yetu kwa watoto tunaowafundisha, tunataka watoto hawa wawe watu wa aina gani? Je wawe na nidhamu ya woga na kutojiamini au wafundishwe tabia ya kutegemeana na yale yanayokubalika na yasiyokubalika.

Kumuongoza mtoto kunahitaji muda na uvumilivu, ni jambo muhimu sana iwapo mzazi anatumia muda fulani katika kuchunguza tabia na mwenendo na kujitahidi kurekebisha kwa upole. Hasira na ukali havisaidii; kama maji yazimavyo moto, upole hurekebisha tabia ya mtoto haraka sana. Tukumbuke pia watoto ni wanafunzi siku zote, wanahitaji uzoefu kutoka kwetu. Ni juu yetu basi kuwapa kilicho bora na muhimu katika uanafunzi wao.

Kawambwa ahimiza ujenzi wa Kiwanja cha ndege Songwe

na Gordon Kalulunga, Mbeya


WAZIRI wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa, amehamasisha ukamilishaji wa Kiwanja cha Ndege cha Songwe, kilichopo mkoani Mbeya, baada ya kutembelea uwanja huo na kuukagua, kisha kuzungumza na mkandarasi na mhandisi mshauri wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini uwanjani hapo.

Kawambwa alitembelea na kuukagua uwanja huo juzi na kuwahimiza Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mkandarasi Kampuni ya Kundan Singh Construction Ltd ya nchini Kenya na mhandisi mshauri kutoka Falme za Kiarabu kuhakikisha ujenzi wa uwanja huo unakamilika mapema iwezekanavyo.

Waziri huyo alisema kuwa kwa sababu awali kikwazo cha uendelezaji wa ujenzi wa uwanja huo kilikuwa ni kutolipwa malipo ya awali mkandarasi anayejenga uwanja huo, lakini kwa sasa tayari serikali imekwisha kulipa deni hilo, hivyo hatarajii kuendelea kusuasua kwa ujenzi katika kiwanja hicho.

“'Kwa sababu serikali imelipa fedha zote za malipo ya awali kwa mkandarasi, hivyo hatutarajii kuona ujenzi wa uwanja huu ukisuasua kama mwanzo, maana kikwazo kilikuwa ni fedha,”' alisema Waziri Kawambwa.

Aidha, alifafanua kuwa ifikapo Januari mwaka 2010 anatarajia kupata taarifa nzuri zaidi za maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambao ni tegemeo kubwa la wananchi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini na taifa kwa ujumla.

“'Kwa kipindi cha mwaka wa bajeti 2008/2009 serikali imetenga sh bilioni 18 kwa ajili ya umaliziaji wa ujenzi wa kiwanja hiki ambacho kina umuhimu sana kwa taifa letu, hivyo ni muhimi pia nanyi kama wataalamu mkaona kuwa ni jinsi gani serikali ilivyoupa kipaumbele uwanja huu,” alisema Kawambwa kwa matumaini ya kumalizika kwa uwanja huo kama matarajio ya serikali yalivyo.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa kiwanja hicho mbele ya Waziri huyo wa Miundombinu kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Prosper Tesha, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi na Uhandisi, White Majula, alisema mkandarasi tayari amemaliza kukata na kujaza udongo njia za kuruka na kutua ndege ambazo waziri alizitembelea na kuzikagua.

“Maeneo yote ya usalama katika njia ya kuruka na kutua ndege yenye urefu wa mita 1,800 tayari mkandarasi ameyakamilisha kwa asilimia 65 na amekamilisha kazi ya ufungaji wa mitambo ya kusaga mawe kwa ajili ya kokoto na ameanza kufunga mtambo wa lami,” alisema Majula.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya uhakika vya habari, imeelezwa kuwa kampuni hiyo kutoka Falme za Kiarabu tayari imelipwa shilingi bilioni 3.1, ambapo kiwango hicho cha fedha kinajumuisha gharama za kazi za kufanya marejeo ya usanifu wa njia za kuruka na kutua ndege pia usimamizi wa utekelezaji wa ujenzi unaoendelea.

Kandarasi ya kumalizia kazi za ujenzi wa kiwanja hicho cha Songwe ilisainiwa Septemba 12 mwaka 2008 na kukabidhiwa Oktoba 19, mwaka huo huo, inatakiwa kazi hiyo ikamilike kwa kipindi cha miezi 18 kwa gharama ya sh bilioni 32.

Tuesday, November 24, 2009

Ufisadi chanzo cha wananchi kupoteza imani kwa CCM

NA MWANDISHI WETU
















Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Yusuf Makamba.

Watanzania wanasifika katika bara la Afrika kwa uvumilivu wao hata nyakati zisizoweza kuvumilika. Dhana hii inaweza kuwa ni matunda aliyotuachia Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Dalili za uvumilivu zinaonekaka wakati wa Utawala wa Serikali ya awamu ya nne. Serikali na viongozi wake wamekuwa wanaendesha serikali kinyemela kana kwamba haikuchaguliwa na wananchi.

Mdororo wa uchumi haukuanza leo katika dunia hii. Tofauti ya mdororo wa uchumi unaotuathiri sasa ni kwamba una miale mikali kuliko midororo ya uchumi iliyopita.

Ni katika mvurugano huu wa uchumi, Watanzania walitegemea kwamba viongozi waliowachagua na hatimaye kuunda serikali wangetafuta mbinu mbadala ili kulinasua Taifa na watu wake ili miale ya mdororo wa uchumi uliopo usingewaumiza sana. Matokeo yake ni kwamba wanaongeza joto la miale na waathirika wa miale hiyo ni Watanzania asilimia 85 waliotopea katika ufukara ndio wanaoumia kwenye joto la mdororo huo.

Wizi uliojitokeza na unaofanywa na vigogo wa Serikali ya CCM ni dalili fika zinazoonyesha kuwa maadili na itikadi iliyozoeleka ya CCM vyote hivyo vimewekwa kando.

Watuhumiwa wote wa wizi wa fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ni vigogo wa CCM na wale wa serikali yake.

Katika orodha hiyo ya watuhimiwa hakuna hata mwananchi mmoja aliye fukara ametuhumiwa na wala hakuna hata mwanachama mmoja wa vyama vya upinzani amediriki kujihusisha na ufisadi.

Ufisadi wote unaozungumzwa ni wa viongozi wa serikali ambao wamefikishwa mahakamani jambo ambalo Watanzania wanaona ni mchezo wa kuigiza.

Watanzania wanaona ni mchezo wa kuigiza kwa sababu vigogo wote waliofikishwa mahakamani ukijumulisha kile kinachodaiwa wameiba haifiki sh. bilioni 133. Hapa panajitokeza swali ambalo halina majibu kwamba hao wengine ambao wanatuhumiwa kinadharia tu watafikishwa lini mahakamani?

Tanzania inashuhudia amani ya mioyo tuliyorithi kutoka kwa Mwalimu Nyerere imetoweka kabisa. Watanzania wanapozungumza amani sio lazima zilie bunduki.

Ukosefu wa amani ni pamoja na kukosa mitaji, kukosa milo mitatu kutwa, dhuluma, rushwa na ufisadi vikiwa mstari wa mbele kuzidi nchi zote zilizo chini ya jangwa la Sahara.

Kukosekana kwa ajira, kuongezeka kwa ujambazi na ujangili si dalili nzuri ya kudumisha amani katika Taifa. Matatizo haya yote yalipaswa kurekebishwa na serikali.

Viongozi wetu wakiwa chini ya mwamvuli wa Rais Jakaya Kikwete hawaonekani kukemea maovu haya ambayo Watanzania hawakuzoe kuwa nayo.

Wazee wetu kama Peter Kisumo, Pancrasi Ndejembi, Joseph Butiku, Mohamed Raza, John Malecela, wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam na Waandishi maarufu kama Jenerali Ulimwengu wao wamekuwa wanayavalia njuga maovu yote yanayovurundwa na viongozi wetu kwa bahati mbaya serikali na chama chake imekuwa haitoi msisitizo ili kuafikiana na mawazo hawa.

Kwa mfumo huu wa falsafa na siasa ambazo ni za nadharia tu zimekuwa hazina tija kwa Watanzania. Hotuba za majukwaani zimekuwa haziendani na vitendo na hatimaye kudumaza usalama katika nchi na kuwaacha Watanzania wakijiuliza, wanakokwenda.

Suala zima katika Taifa ni kwamba nchi haina amani kwa sababu, wananchi hawana mlo uliokamilika, mafukara wa kutupwa wakati viongozi wao wanajinafasi kana kwamba wako mbinguni, usalama majumbani umekuwa haupo kwa sababu ya ujambazi uliokirithiri na polisi ina vitendea kazi duni ukifananisha na silaha zilizomo mikoni mwa majambazi.

Tatizo jingine Taifa halijaongeza ajira kwa polisi. Polisi tuliyonayo sasa ni ileile aliyotuachia Mwalimu Nyerere.

Kukosekana kwa utawala bora katika Taifa kumeathiri sana suala zima la usalama katika nchi. Watendaji wa tarafa, mitaa, vitongoji na kata wamekuwa tishio kubwa kwa usalama wa Raia.

Watendaji hawa wanajiita watunza usalama madaraka ambayo hata katika Katiba ya nchi hayapo. Kwa mshangao wa Watanzania wengi watendaji wamekuwa wanachukua sheria mikononi huku wakijua sio stahili yao, lakini wakuu wa mikoa na wilaya licha ya kushindwa kukemea, wamekuwa hawawachukulii sheria za nidhamu hivyo kuhalalisha vitendo vibaya vinavyofanywa na watendaji hao. Ukosefu wa utawala bora na sheria katika Taifa ndio umehatarisha usalama wa nchi.

Dhana ya kudumisha demokrasia endelevu katika Taifa haipo. Serikali pamoja na CCM kama alivyosema Rais Kikwete wakati wa kuadhimisha miaka kumi ya kifo cha Mwalimu Nyerere ni kwamba viongozi wameacha kabisa kusikiliza kero za wananchi na kuwasaidia.

Kinachobaki sasa ni porojo nyingi za siasa zisizokuwa na tija na kujilimbikizia mali ili kuja kugombea uongozi mwaka 2010.

Wanasiasa wengi wamebadili dira na maendeleo ya kisiasa na hatima yake wamegeuza siasa mradi wa kujinufaisha wao na familia zao.

Kwa sababu wakati wanagombea hivyo vyeo vya siasa wanatumia rushwa kwa hiyo wakivipata wanahakikisha fedha yao yote iliyotumika katika rushwa inarudishwa kwa nyakati mbalimbali. Hii ina maana kwamba, maendeleo ya wapiga kura yanawekwa pembeni.

Watanzania ambao kusema kweli wamechoshwa na siasa za CCM zenye poroja nyingi na zisizokuwa na tija. Ili wajinasue kutoka kwenye matatizo hayo wanadhani ni wakati muafaka wa kukiweka Chama Cha Mapinduzi na watafute ustarabu mwingine ambao pengine unaweza ukaleta neema ambayo itawanufaisha wao na vizazi vijavyo.

Suala ni kwamba Siasa za Tanu na CCM zimekuwa katika Tanzania kwa miaka 48 bila maendeleo yoyote kwa wananchi.

Tutaboreshaje elimu katika shule za serikali?

BY BENJAMIN NKONYA

Chimbuko la maendeleo ya elimu nchini ni matokeo ya michakato ya sheria, falsafa na sera zilizoanzishwa katika vipindi mbalimbali kabla na baada ya uhuru. Baada tu ya kupatikana uhuru mwaka 1961, serikali ilitunga sheria ya elimu namba 83 ya mwaka 1962 iliyofuta sheria ya elimu ya mwaka 1927 ambayo iliruhusu utoaji wa elimu na mafunzo kwa mfumo wa ubaguzi wa rangi, dini na makabila.

Katika sheria hii, serikali iliekeza mitaala, uongozi na ugharamiaji wa elimu na mafunzo ufuate usawa. Azimio la Arusha la mwaka 1967 lilianzisha falsafa ya elimu ya kujitegemea ambayo ilisababisha mabadiliko makubwa katika sera za jumla za kijamii na kiuchumi.

Falsafa hii, ambayo iliasisiwa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ndiyo inaweka dira katika mfumo wetu wa elimu hadi leo, inaweka mkazo katika kuondoa matabaka kwenye utoaji wa elimu, utengano (alienation) kati ya shule na jamii na kusaidia kuondoa kasumba ya wasomi ya kujibagua na kutumia elimu waliyoipata kwa manufaa yao binafsi.

Aidha falsafa hii inaelekeza katika kuunganisha nadharia na vitendo, kwa dhana kuwa elimu isipatikane vitabuni tu bali ijumuishe na ile ipatikanayo kutokana na uzoefu wa kutenda au kufanya kazi ya kuongeza tija.

Ili kuhakikisha kwamba haya yanafikiwa na pia kuhakikisha kwamba wanafunzi wanawajibika na upatikanaji wa mahitaji yao, falsafa hii inaelekeza shule kuwa vituo vya kuzalisha mali ili kuchangia gharama za uendeshaji kwa asilimia ishirini na tano. Pia elimu inayotolewa katika ngazi zote iwe na maarifa na stadi za kumwezesha mhitimu kuishi na kufanya kazi yenye manufaa katika jamii.

Katika kutekeleza falsafa hii, shule karibu zote zilitaifishwa na kuendeshwa na serikali kuanzia mwaka 1967. Ili kuondoa aina zote za ubaguzi, serikali ilikubali kugharamia elimu katika ngazi zote. Pamoja na hayo, kila shule ilianzisha mashamba ambayo yalikuwa maarufu kama mashamba ya elimu ya kujitegemea. Hali hii ilimfanya mwanafunzi wa Kitanzania kuwa tayari kujitegemea mara tu baada ya kuhitimu mafunzo ya elimu ya msingi. Kwa hakika falsafa hii ilishabikiwa sana na kila Mtanzania.

Pamoja na uzuri wa falsafa hii, kuna changamoto zilizoukabili mfumo mzima wa elimu katika miaka kumi ya utekelezaji wa falsafa hii. Kama wote tunavyofahamu, katika nusu ya pili ya miaka ya 1970, ubora wa elimu yetu ulishuka sana kiasi kwamba serikali iliruhusu walimu wasio na sifa kuanza kufundisha katika shule za msingi.

Changamoto hii iliambatana na ukosefu wa zana za kufundishia na kujifunzia kama vitabu, maabara, maktaba n.k. Sambamba na changamoto hii, ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi halikuenda sambamba na ongezeko la idadi ya vyumba vya madarasa na samani zake, achlia mbali nyumba za waalimu.

Hivyo ililazimu chumba kimoja cha darasa kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi kuliko idadi inayomfanya mwalimu alimudu darasa kiufundishaji. Pamoja na changamoto hizo, hata suala la usimamizi wa elimu nalo lilikuwa gumu kutokana na shule kuwa nyingi katika mtawanyiko wa kijiografia ambao una ufanisi mdogo. Matokeo ya hali hii ilikuwa ni kushuka kwa elimu kwa haraka sana.

Serikali iling’amua changamoto hizi na kutafuta namna ya kuziondoa ili elimu iendelee kutolewa kwa ubora unaotegemewa. Mwaka 1978 Bunge lilitunga sheria mpya ya elimu namba 25 ambayo, pamoja na mambo mengine, iliruhusu watu binafsi, mashirika ya dini, asasi za kiraia na makampuni kuanzisha, kusajili na kuendesha shule.

Kuanzishwa kwa sheria hii kulianza kuonyesha matumaini ya kunusuru ubora wa elimu kwani shule nyingi binafsi zilionyesha mafanikio. Kuna changamoto kadhaa ambazo zilijitokeza katika miaka kumi na tano ya kwanza ya utekelezaji wa sheria hii.

Changamoto hizi zilirekebishwa kupitia sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995. Hivyo mfumo wetu wa sasa wa utoaji wa elimu na mafunzo nchini unaongozwa na sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995 (iliyopata nguvu kutokana na marekebisho ya sheria ya elimu Na. 25 ya mwaka 1978 iliyorekebishwa kwa sheria Na. 10 ya mwaka 1995), sera ya elimu ya ufundi ya mwaka 1996 na sera ya elimu ya juu ya mwaka 1999.

Pamoja na ukweli kwamba shule za serikali zinaendeshwa kwa kodi za Watanzania pamoja na ufadhili mwingi sana kutoka mashirika mbalimbali ya ndani nje ya nchi, elimu yetu, hasa inayotolewa na shule za serikali, bado ina changamoto nyingi sana katika viashiria vya utoaji (input), mchakato (process) na matokeo (outputs).

Baada ya marekebisho hayo na baada ya sekta binafsi kujiimarisha ipasavyo, Watanzania wameendelea kushuhudia kukua kwa haraka sana kwa elimu katika sekta binafsi licha ya ukweli kwamba shule hizi hazina ruzuku yoyote kutoka serikalini. Sasa ni zaidi ya miaka thelathini tangu kuruhusiwa kwa sekta binafsi kuingia katika utoaji wa elimu.

Pengine ingekuwa busara kudurusu sababu hasa za tofauti hizi na kutafuta namna ambavyo elimu yetu katika sekta ya umma inaweza kuboreshwa.

Ni ukweli usionpingika kwamba gharama za uendeshaji katika shule za serikali ni kubwa kuliko gharama katikashule binafsi. Hii inatokana na ukweli wa kiuchumi kwamba kadri mradi unavyozidi kuwa mkubwa ndivyo ufanisi kwa kila shilingi inayotumika unavyozidi kushuka. Hali hii inakabili vilivyo shule zetu za serikali.

Moja ya viashiria vya kushuka kwa ufanisi ni hii hali ya waalimu kuwa na malalamiko yasiyoisha kuhusu mapunjo wanayopata katika malipo yao, baadhi ya wanafunzi kuvuka madarasa na vidato bila kujua kusoma na kuandika, kukosekana kwa maabara, maktaba, vitabu na vifaa vingine vya kujifunzia na kufundishia na mambo mengine yanayofanana na hayo.

Sababu nyingine za kudorora kwa elimu katika shule za serikali ni kuingiliwa kupita kiasi na wanasiasa. Utakuta taarifa ya wakaguzi inaonyesha kabisa kwamba shule fulani haitakiwi kusajiliwa kutokana na kutotimiza baadhi ya vigezo vya usajili. Pamoja na taarifa hizo, utakuta mwanasiasa anaingilia kati na kulazimisha shule hiyo isajiliwe.

Hivyo hata uendeshaji wake huenda kisiasa siasa tu bila kujali vigezo muhimu vya uendeshaji wa shule. Utakuta shule ya serikali imesajiliwa lakini haina hata kitabu kimoja wala maabara. Itakuwa ni ajabu isiyo kifani kukuta shule kama hii ikitoa elimu bora.

Hali ni tofauti kabisa katika shule binafsi. Shule hizi husimamiwa na kwa ukaribu sana. Shule hizi hukaguliwa na kusajiliwa baada ya kutimiza vigezo vyote vya usajili. Huwezi kukuta shule binafsi inasajiliwa wakati haina maktaba yenye vitabu au maabara zenye vifaa vyote. Hata baada ya usajili, wakaguzi hufika katika shule hizi mara kwa mara kuangalia kama kila kigezo cha utoaji wa elimu kinazingatiwa.

Sambamba na hili, utakuta mmiliki wa shule hizi anafuatilia kwa karibu sana kila kinachoendelea shuleni na kuhakikisha wanafunzi wake wanapata huduma zinazotakiwa.

Kwaujumla wake ni kwamba shule binafsi huendeshwa kwa kufuata mahitaji ya wateja wake na kutimiza masharti yote yanayowekwa na serikali.

Kurunzi haioni kama itatosha tu kukosoa bila kutoa mapendekezo ya ubereshaji. Njia ya kwanza ni kuondoa siasa katika uendeshajiwa usajili na uendeshaji wa shule.

Hii inaweza kufikiwa kwa njia ya kuifanya idara ya ukaguzi kuwa wakala inayojitegema badala ya hali iliyopo ya kuwa idara katika Wizara Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Itakuwa ni ajabu ya ngariba kujitia suna mwenyewe kama kitengo hiki kitatenda haki hasa wakati shule ya serikali inapofanya makosa.

Njia ya pili ni kuweka ushirikiano kati ya wamiliki wa shule binafsi na serikali ili kuondoa tatizo la kushuka kwa ufanisi wa usimamizi unaotokana na kukua kwa idadi ya shule zinazosimamiwa na mmiliki mmoja.

Katika hali hii, mmiliki wa shule binafsi anaweza kuwekwa kuwa meneja wa shule ya serikali (hasa hizi za kata) iliyo karibu naye. Kama meneja, atahakikisha kwamba anashirikiana na bodi ya shule katika kuhakikisha kwamba shule hii ya kata inatoa elimu bora kama ilivyo shule yake.

Elimu ni mali ya umma na inatakiwa kugharamiwa na umma hata kama inatolewa na shule/chuo binafsi. Kurunzi inaamini kabisa kwamba, tukilizingatia hili, tutakuwa tumekata kabisa mizizi yote ya ufisadi dagaa, papa na nyangumi na tutakuwa tumeenzi na kuhuisha fikra sahihi za Baba yetu wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.