Thursday, November 26, 2009

Dk Salim: Ukiona nchi ina matatizo, wa kulaumiwa ni viongozi

Hawra Shamte


Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) Dk Salim Ahmed Salim ambaye ameeleza kuwa nchi inapokuwa na migogoro mingi wanaostahili kulaumiwa ni viongozi.


JITIHADA mbalimbali zinafanyika kuhakikisha kuwa nchi za Kiafrika zinafuata utawala wa sheria na pia kuzingatia haki za binadamu.

Mbali na nhi wahisani, nchi zilizoendelea na hata mashirika ya umoja wa mataifa kusisitiza umuhimu wa utawala wa sheria na haki za binadamu, zipo taasisi huru zilizo ndani ya nchi za Kiafrika ambazo nazo zinashajiisha uwepo wa utawala bora katika nchi za Afrika.

Mojawapo ya asasi za namna hiyo ni taasisi ya Mo Ibrahim ambayo mwanzilishi wake ni Dk Mohamed Ibrahim mzaliwa wa Sudan na tajiri aliyejikita katika masuala ya mawasiliano.

Mjumbe wa bodi ya taasisi ya Mo Ibrahim, Dk Salim Ahmed Salim anasema tatizo la nchi nyingi za Afrika ni ukosefu wa Utawala Bora, katika Makala hii, Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) Dk Salim aliyezungumza na mwandishi wetu HAWRA SHAMTE anaeleza jinsi ukosefu wa utawala bora unavyokinza demokrasia barani Afrika...

Swali: Bara la Afrika linakabiliwa na matatizo mengi ya kivita, ya kiuchumi, ya kisiasa na ya kijamii.

Mwasisi wa taasisi ya Mo Ibrahim, Dk Mohamed Ibrahim, raia wa Sudan hivi karibuni alizungumza katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam na kusema kwamba tatizo kubwa la nchi za Kiafrika ni ukosefu wa utawala bora, lakini dhana ya utawala bora ni pana sana, je, wewe unazungumza nini kuhusu dhana hii?

Jibu:Hakuna asiyetambua kuwa Bara hili lina nyenzo nyingi sana, lina kila aina ya mali, rasilimali yetu kubwa kuliko zote ni watu wetu ambao wanafanyakazi usiku na mchana tena katika mazingira magumu.

Kuna kila aina ya madini katika bara letu, dhahabu almasi na kadhalika, pamoja na hayo tuna mafuta pia katika bara letu. Kuna ardhi kubwa sana katika Afrika, kuna mito na maziwa ya kila aina lakini bado nchi zetu, watu wetu ndio wenye umasikini kuliko watu wote duniani.

Kwanini inakuwa hivyo? Kwa kweli hii inatokana na uongozi, kwa hiyo suala la uongozi bora ni suala la msingi, pale ambapo uongozi wa nchi umekuwa na uwezo wa kuhakikisha kwamba wanashughulikia maslahi ya watu wao, kunakuwa na tofauti kubwa.

Katika utoaji zawadi kwa viongozi bora, mchakato unaofanywa na taasisi ya Mo Ibrahim tunaangalia kiongozi alifanya nini kuboresha hali ya watu wake wakati akiwa madarakani.

Bara letu lina matatizo ya kiuchumi, lina matatizo ya rushwa kubwa sana, lina matatizo ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, lina matatizo ya uvunjaji wa haki za binadamu.

Taasisi ya Mo Ibrahim inachofanya ni kusaidia mchakato wa kidemokrasia na utawala bora, kwani si kweli kama bara la Afrika ni matatizo tu, si kweli kwamba kila nchi ya Afrika inanuka rushwa.

Kwa kweli kuna juhudi kubwa zinafanyika katika bara letu na mchakato wa kidemokrasia umepiga hatua nzuri pamoja na kwamba mwaka jana na mwaka huu tumepata misukosuko kidogo; matukio ya Guinea kwa mfano ambako wananchi wanauliwa na utawala wa kijeshi, matukio ya Mauritania, matukio ya Guinea Bissau na halafu zaidi matukio ya Somali na matukio ya Sudan.

Kwa mfano Sudan siyo suala la Darfur tu lakini ni nini mustakabali wa Sudan na nini itakuwa taathira ya mambo yanayotokea Sudan kwa bara letu la Afrika.

Kote unapoona kunakuwa na matatizo, kwa kweli wa kulaumiwa kwanza ni uongozi. Pale panapokuwa na uongozi safi, unaojitolea, uongozi usioshiriki ufisadi, uongozi unaojali zaidi maslahi ya watu wake, gurudumu la maendeleo linasonga mbele, lakini pale ambapo viongozi wanajilimbikizia mapesa, wanafanya mambo ya kidikteta na kadhalika, nchi hiyo hata ikiwa na nyenzo vipi haiwezi kwenda mbele.

Swali: Umeeleza kuwa katika maeneo yenye matatizo kama vile ya kivita ni ukosefu wa uongozi, lakini je, nchi kama Somalia ambayo wanapigana wenyewe kwa wenyewe na mpaka sasa inaitwa nchi isiyokuwa na dola je, tatizo ni hilo tu la kukosa uongozi bora?

Jibu:Ukitazama sana matatizo ya Somalia utaona kuwa ni ukosefu wa uongozi. Wanaopigana Somalia hivi sasa ni watu na wanaopata matatizo makubwa ni wananchi wa kawaida. Majemedari wa kivita ni viongozi mbalimbali wa Somalia na hawa walichofanya ni kuweka maslahi yao mbele kuliko maslahi ya watu wao.

Kama kuna nchi ya Kiafrika ambayo haikutegemewa kuwa na matatizo kama haya ilikuwa ni Somalia kwa sababu ni nchi ambayo watu wake wana dini, moja, wana utamaduni mmoja na wanazungumza lugha moja, isingetegemewa kuwa watu kama hao itatokea siku watapigana wenyewe kwa wenyewe, familia moja inaua familia nyingine.

Tatizo la Somalia ni ukosefu wa uongozi bora unaofikiria maslahi ya watu wake, lakini tatizo hilo si la Somalia tu, tazama Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) ni nchi moja ambayo pakiwa na utulivu, pakiendeshwa utawala bora itakuwa ni chachu ya maendeleo siyo ya Kongo tu bali ya sehemu kubwa sana ya bara la Afrika.

Lakini Kongo haikupata amani kwa muda mrefu sana, ingawa hivi sasa Rais Kabila anajitahidi kujaribu kuleta amani kwa kiwango kikubwa lakini bado kuna vita vya wenyewe kwa wenyewe, bado kuna watu wanafikiria maslahi yao, namna gani ya kupata fedha kwa njia za haramu kuwa ni jambo kubwa zaidi kuliko jambo jengine.

Swali: Unafikiri ni nini suluhisho la matatizo haya?

Jibu: Sidhani kama unaweza kuwa na suluhisho la namna moja kwa sababu kila pahala na mazingira yake.

Chukulia Somalia kwa mfano, Somalia kuna Al Shabab, hawa wanasema wao ndio Waislam safi na wanataka kuleta Uislam, lakini ni upuuzi mtupu, kwa sababu haiwezekani kuwa brandi yako tu ya Uislam ndiyo iwe bora kuliko nyingine hufiki mbali.

Lakini pia Somalia ilipuuzwa, baada ya matatizo yaliyotokea Mogadishu wakati wa Jenerali Aideed na Marekani kupata msukosuko; wanajeshi wa Kimarekani waliingia kwa dhamira ya kutoa misaada ya kibinadamu 'humanitarian' halafu humanitarian ikabadilika wakaanza kuingia katika mapambano, askari wa Kimarekani wakauliwa katika helikopta yao na wakaburutwa; toka wakati ule Marekani iliitenga kabisa Somalia.

Nakumbuka nilipokuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Afrika, nikienda Marekani naweza kuzungumza tatizo lolote lakini si Somalia, ilikuwa ukitaja Somalia wanakwambia achana nao hao.

Kwa hivyo ni nchi ambayo ilitengwa, Marekani waliitenga lakini na jamii kubwa pia waliitenga, tukaiachia inaendelea tu…

Jingine ni kuwa viongozi wa nchi ile wakaanza kugawana; Somalia iliyokuwa jamii moja, wakaanza kugawana sasa kuna makabila, ukoo, familia na kadhalika. Ingawa hivi sasa Somalia kuna juhudi zinafanyika lakini juhudi zozote zinazofanyika lazima waishirikishe Al Shabab. Huwezi kupata ufumbuzi wa kivita pale lazima pawe na mazungumzo ya dhati kabisa…

Kwa DRC juhudi kubwa imefanyika, hali iliyoko DRC sasa hivi tofauti sana na miaka mitatu, minne, mitano iliyopita lakini bado kuna matatizo Mashariki ya Kongo, kwanini? Moja ya matatizo yetu katika bara letu, imekuwa hizi rasilimali tulizonazo, nyenzo tulizonazo, madini tuliyonayo baada ya kuwa faida kwa watu wetu imekuwa kama ni dhambi, kama ni laana, sasa inakuwa pale palipo na mafuta matatizo, palipo almasi matatizo, palipo dhahabu matatizo, mimi nadhani changamoto kubwa ya bara letu ni namna gani ya kugeuza hizi rasilimali, hizi nyenzo tulizonazo, baada ya kuwa ni sehemu ya matatizo iwe ni sehemu ya kuleta maendeleo kwa bara zima na kwa manufaa ya watu wetu.

Kwa upande wa Sudan kwanza tatizo lilikuwa baina ya Kaskazini na Kusini, vita viliendelea kwa muda mrefu sana na watu wengi walifariki, takwimu zinasema watu kama milioni nne walifariki katika vita vya wenyewe kwa wenyewe baina ya Kaskazini mwa Sudan na Kusini mwa Sudan.

Mwaka pale. Mwaka 2005 yakapatikana makubaliano ya kijumla (Comprehensive agreement).

Halafu kuna suala la Darfur, huko nako kuna matatizo makubwa, mpaka hivi sasa juhudi zilizofanyika kujaribu kutanzua hazijafanikiwa.

Lakini hivi sasa hali ya Sudan imekuwa ngumu zaidi na mimi binafsi inanitisha kidogo, inanitisha kwa sababu siyo tu suala la Darfur lakini kuna uwezekano wa kuwa na fujo zaidi kama ndugu zetu wa serikali ya Sudan ya Kaskazini na ndugu zetu wa SPLM hawakuwa na makubaliano ili kura ya maoni ya mwaka 2011 ikafanyika katika mazingira mazuri na halafu wakaheshimu matokeo ya kura ile.

Tatizo lililopo hivi sasa inaonyesha kuwa badala ya kuwa na umoja wa Sudan kuna uwezekano kuwa watu wengine wakataka kujitenga.

Najua kama kuna watu wengine wanafurahia kujitenga, wanasema kujitenga ni nzuri, lakini ukianza suala la kujitenga katika bara letu na hasa katika nchi kubwa kama Sudan kuna taathira zinazoweza kutokea siyo tu ndani ya Sudan lakini pia katika majirani wa Sudan.

Kwa hiyo mimi nafikiri hili jambo la Sudan kwa sasa Jumuiya ya Kimataifa na hasa nchi za Kiafrika zinapaswa kulipa uzito wake na kujaribu kuhakikisha kwamba katika huu muda uliobakia kila jitihada zinafanywa ili kuwafanya wananchi wa Sudan wajione kuwa ni wamoja na hasa ambao wanahisi kwamba wameonewa.

Tatizo kubwa la Sudan ni kwamba wananchi walio katika pembezoni wanahisi kwamba wametengwa (siyo kama hawana sababu) na maslahi yote na maendeleo yote yanatokea katika sehemu moja tu ya Sudan.

Jambo moja ambalo linaweza kuwa zuri ni kujaribu kuibana serikali ya Sudan kuzungumza na ndugu zetu wa SPLM waandae mazingira ili wananchi wa Kusini mwa Sudan watakaopiga kura waseme kwamba jamani tuhakikishe hili suala la umoja linapatikana.

Lakini kama hilo halipatikani basi angalau waandae mazingira ya kuwa huo mchakato wa kura za maoni uwe wa amani na wakubaliane na mapema kama kuna kura ya maoni likitokea hili tutafanya nini, lisiachwe tu kama bomu likapasuka kwa sababu kama hakuna hivyo kuna hatari kabisa kwamba ufikapo mwaka 2011 bila mawasiliano,

bila mapatano bila ushirikiano hali ya Sudan ikaendelea kuwa tete na inapoendelea kuwa tete haitokuwa tu Kusini mwa Sudan lakini itaathiri pia sehemu mbalimbali za Sudan ambazo pia zina matatizo yake, Darfur, Kordufan, Blue Nile na kadhalika.

Swali: Kumezuka mtindo mwengine wa demokrasia barani Afrika, sasa hivi demokrasia mbali ya kuwa ni mchakato wa uchaguzi lakini mwisho wa siku inabidi lazima watu wakae katika meza za majadiliano. Na zimezuka hizi serikali za mseto kama Kenya na Zimbabwe, je, nini maoni yako kuhusu hilo?

Jibu: Kila sehemu ina mazingira yake maalum. Demokrasia maana yake ni kwamba wananchi wenyewe wawezeshwe kuchagua viongozi wao na namna serikali wanayoihitaji na serikali hiyo iwaongoze kwa muda gani na wawe na uwezo wa kubadilisha viongozi wao muda ule unapofika.

Lakini mazingira yatofautiana, kwa mfano; katika Kenya baada ya mauaji yaliyotokea mara baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 na kuleta taathira kubwa kwa maendeleo ya Kenya kulikuwa na umuhimu wa kutafuta usuluhishi na mawasiliano na maafikiano ya namna fulani, kwa hivyo serikali ya mseto iliyoundwa Kenya, ilikuwa na madhumuni hayo.

Ukitazama mazingira yalivyokuwa, ukawa mkaidi tu ukasema hakuna haja ya kuwa na serikali ya pamoja kwa kweli unakosea, unawatakia ndugu zetu wa Kenya waendelee katika maafa tu.

Zimbabwe kidogo tofauti na Kenya, lakini kama wenyewe wamekubaliana, tunapaswa kuheshimu makubaliano. Ukitazama uchaguzi wa Zimbabwe ulivyokwenda, Chama cha MDC katika uchaguzi wa wabunge kilishinda, suala lilikuwa je, uchaguzi wa Rais ulikuwaje? Bahati mbaya mazingira hayakuwa yanaruhusu kufanya uchaguzi ambao ungekuwa huru na wa haki.

Kwa hivyo katika mazingira kama hayo, mimi nadhani ilikuwa ni busara kujaribu kuwakutanisha viongozi ili waweze kuona jinsi ya kuwa na muundo wa serikali ambao utazingatia maslahi ya watu wote wa Zimbabwe.

Na pamoja na kuwa bado kuna matatizo nchini Zimbabwe, lakini nadhani hilo lilikuwa ni jambo la busara. Mimi nadhani pale ambapo kuna ushindani mkubwa sana wa kisiasa na ambapo bado watu hawajaweza kustahmiliana na kuweza kujua kuwa wewe unaweza ukawa chama fulani, mimi nikawa katika chama kingine, hata katika familia moja; baba akawa chama fulani, mama akawa chama kingine na watoto wakawa chama kingine na mkaendelea katika familia bila matatizo; pale ambapo ustahmilivu kama huo haupo.

Ni muhimu sana kufanya utaratibu wa kushirikisha watu wote katika utawala, vinginevyo utaendelea katika mapambano tu na panapo mapambano ni muhali kupata maendeleo ya kudumu ya kiuchumi.

Jamani hatupungi mashetani hapa, tunasoma

Na Brandy Nelson, Chunya




Wanafunzi wakiwa darasani wakiendelea na masomo


HADI kufikia mwaka 2000 kijiji cha Udinde kilikuwa na shule moja ya msingi iitwayo Udinde iliyochukua watoto kutoka vitongoji vya jirani pia, lakini ulipoanzishwa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (Mmem) mwaka 2002 ilionekana haja ya kufanya maboresho.

Shule hiyo ilipachuliwa ikazaa shule nyingine ya msingi katika kitongoji cha Iboma mwaka 2003.

Uamuzi wa kujenga shule nyingine, mbali ya kufanya maboresho ulilenga pia kuwapunguzia wanafunzi adha ya kutembea umbali wa kilomita 10.

Serikali ya kijiji hicho kilichopo kata ya Kapalala tarafa ya Kwimba wilaya ya Chunya mkoani Mbeya ikitumia pesa zilizotokana na Mmem ilifanikiwa kujenga darasa moja tu na hadi sasa halijakamilika wala halijaongezwa darasa jingine wala vyoo na nyumba za mwalimu.

“Shule hii ilimegwa kutoka shule ya msingi Udinde ambapo hapa Iboma tuliletwa walimu watatu na mazingira yenyewe ni kama haya unavyoyaona. Wazazi walichangia kujenga darasa hili moja na serikali kupitia Mmem ikamalizia paa ingawa darasa lenyewe bado halina sifa ya kuwa darasa kwani halijakamilika,” anasema mwalimu Albert Juakali ambaye alikutwa akifundisha hisabati wanafunzi wa darasa la kwanza.

Uamuzi wa haraka uliofanywa na walimu ni kuhamishia ‘mikoba’ yao kwenye mti wa mbuyu ulio jirani na kuweka mbao. Upande mmoja wanakaa darasa la kwanza, halafu upande mwingine darasa la pili, la tatu, la nne, la tano nk. Wakati wa juakali shida na wakati wa mvua ni likizo.

Mwenye masikitiko zaidi ni mwalimu mkuu wa shule, Onesmo Mdamu ambaye anasema;"Sikiliza, shule hii ina muda wa miaka sita mpaka sasa lakini ina darasa hili moja tu na ambalo linatumika kwa ajili ya watoto wa darasa la sita na hawa wa madarasa mengine wanasoma kwenye mti wa mbuyu ambao pale kuna madarasa matano yaani la kwanza, pili, tatu, nne na tano kama mnavyoona wenyewe."

Hayo ndiyo maisha ya wanafunzi wa shule hiyo na uamuzi wa kutumia mti huo kama darasa ulipitishwa na kamati ya shule.

Madhara

Mazingira hayo yamewasaidia zaidi watoto wasiopenda elimu maana huona heri kwenda kujishughulisha na uvuvi wa samaki kwenye Ziwa Rukwa lililojirani na shule hiyo badala ya kushinda kwenye juakali chini ya mti.

"Mazingira ya shule hii ni magumu kutokana na kuwa na darasa moja ambalo linatumiwa na wanafunzi wa darasa la sita. Shule yenyewe kama unavyoiona iko kandokando ya Ziwa Rukwa hivyo inapelekea watoto kuamua kujishughulisha na ajira ya uvuvi wa samaki kutokana na mazingira magumu ya shule na ugumu wa maisha wa familia zao na hivyo kukosa haki ya kupata elimu bora," anaongeza Juakali.

Aliyeamua kubadili matumizi ya mbuyu kutoka kwenye imani za asili kwamba ni makazi ya mashetani hadi kuwa darasa la wanafunzi 134 ni kamati ya shule. Kamati hiyo ya shule imeshindwa kuhamasisha wananchi yajengwe madarasa mengine.

Kinachofanyika chini ya mti wa mbuyu, Mdamu anasema wanafunzi huchukua mabanzi na kuweka juu ya matofali na sehemu ya kuandikia wakitumia matofali kama meza na wengine wakishindwa kupata mabanzi hutumia matofali kama viti.

"Hali hii ni mbaya kielimu kwani hata sisi walimu hatujui tumwachie nani hawa wanafunzi, basi tumeona tuungane na usemi usemao 'Ualimu ni Wito', lakini kwa ujumla hali ni mbaya sana. Hata mahudhurio ya wanafunzi ni finyu kutokana na kukatishwa tamaa na mazingira na kupelekea kujiingiza katika shughuli za uvuvi wa samaki,” anasema

Mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo, Leopard Ngairo mbali ya kuelezea historia anakiri kwamba mazingira ya ufundishaji ni magumu na yanachangia wanafunzi kukosa elimu bora na hivyo wengine kuamua kuacha shule na kujiingiza katika ajira ya shughuli za uvuvi wa samaki.

"Shule ina darasa moja pekee, ina uhaba wa madawati, ofisi za walimu, vifaa vya kufundishia hakuna ambapo kwa sasa shule ina vitabu viwili kwa kila darasa, kwa kweli walimu wanashindwa kutoa elimu ipasavyo kwa wanafunzi," anasema Ngairo.

“Hii shule ina matatizo makubwa huwezi kufananaisha na shule zingine kwani wazazi wengi wanakatishwa tamaa na mazingira yake na inasababisha wazazi kuwaruhusu watoto wao kutafuta ajira katika shughuli za uvuvi badala ya kwenda shule,” anasema

Darasa la saba

Septemba mwaka huu walimu na kamati ya shule walisugua vichwa kuona namna nzuri ya kuwasaidia wanafunzi wa darasa la saba waliotarajiwa kufanya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi. Hapo tena, walimu na kamati ya shule walikubaliana kulihamishia darasa hilo Udinde kwa ajili ya kumalizia elimu yao ya msingi.

"Hapa kwa kweli hakuna elimu bora inayopatikana kwani mazingira yote kwa ujumla ni magumu siyo kwa wanafunzi wala sisi walimu kwani hakuna hata vitendea kazi na tunaishi mbali na shule na inatulazimu kutembea umbali wa kilometa tisa ili kuweza kufika hapa shuleni," anasema Mdamu.

Mahitaji ya shule hiyo ni kuwa na walimu watano lakini waliopo wanaofanya kazi ni wawili pekee, hakuna vitabu vya kufundishia kwani vilivyopo ni vitabu viwili kila darasa na kwamba madawati ni tatizo kubwa hali inayopelekea watoto hao kukaa kwenye matofali.

Walimu hao wamekuwa wakifundisha kwa moyo wote na wamekuwa wakipeleka ripoti kila mwezi kwa afisa elimu wa halmashauri kuwajulisha hali halisi ya shule, lakini hakuna kinachofanyika na kuifanya shule hiyo kutokuwa na maendeleo yoyote.

Mdamu analalamika pia kwamba hali hiyo kwa kiasi fulani inachangiwa na baadhi ya wazazi katika kitongoji hicho kukosa mwamko wa kuwapeleka watoto wao shule na badala yake wamekuwa wakijikita zaidi kwenye shughuli za uvuvi kuliko suala la elimu kutokana na mazingira ya shule hiyo.

Mwalimu mkuu anadhani kwamba ufumbuzi wa haraka juu ya matatizo ya shule umo kwenye mikono ya viongozi wa wilaya na mkoa.

"Kama viongozi wa serikali ya wilaya na mkoa wangetembelea na kushuhudia mazingira ya shule na kuwahamasisha wananchi wajitolee nguvu zao kujenga shule ni jambo ambalo lingesaidia watoto hao kupata elimu bora badala ya bora elimu ambayo wanaipata kwa sasa," anasema.

Wanafunzi nao wamefikia hatua ya kuuona ukweli kwamba hakuna wanachopata katika mazingira kama haya. Adela Alex, mwanafunzi wa darasa la sita anasema mazingira ya shule hiyo ni magumu na hivyo kupelekea kushindwa kupata elimu bora na kusabibasha baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo kukatamaa na kuendelea na shule na kujiingiza katika shughuli za uvuvi wa samaki kwa kufanya vibarua na kujipatia fedha kidogo.

"Kwa kweli sisi wanafunzi tunaona hali hii ni mbaya kwetu tunaona kama tumetengwa labda sisi siyo raia wa Tanzania au labda serikali inatuona kama wanyama, haiwezekani tukawa tunasoma shule katika mazingira haya ya chini ya mti wa mbuyu halafu tukasema kuna kitu tunakipata; hakuna tunachokipata hapa chini ya mti,"anasema kiongozi wa wanafunzi Emanuel Mkombe.

Anasema kuwa mazingira hayo hayawawezeshi kusoma vizuri yanawakatisha tama ndiyo maana kuna baadhi ya wanafunzi wamekimbia na kuamua kufanyakazi ya vibarua ziwani. Lakini kuna wanafunzi wengine ambao wana nia ya kusoma ndiyo maana wameendelea kuwa wavumilivu na kukubali kusoma chini ya mti wa mbuyu.

Mkombe anasema kuwa kuna hatari ya wanafunzi wote wasichana kwa wanaume kukimbilia ziwani kwa ajili ya kupata ajira katika shughuli za uvuvi ambako wanalipwa fedha kidogo kuanzia kati ya Sh 500 hadi Sh 200 kwa kazi wanazopewa ikiwa ni pamoja na kupasua samaki, kutafuta kuni, kuosha nyavu na kukausha samaki.

Anasema kuwa ajira hiyo ni mbaya kwa watoto na ni hatari kutokana na wengi wao kupata ajali mbalimbali ziwani ikiwa ni pamoja na kukamatwa na mamba na kupoteza maisha bado wakiwa na umri mdogo.

"Tunaiomba Serikali iliangalie suala hili la mazingira ya shule yetu ili na sisi tuweze kupata haki ya kupata elimu kama wanavyopata wenzetu ili tuweze kuokoa maisha yetu na kujinusuru na ajira hii mbaya ya watoto katika Ziwa Rukwa kwani sidhani kama kuna watoto wenzetu wengine wanasoma katika mazingira kama haya," anasema.

Mtazamo huo ndio alionao Ngairo kwamba: "Kama unavyoona tunaendelea kuomba wananchi na wadau wa Elimu kutuchangia ujenzi wa shule yetu na na sasa tumeanza kujenga darasa lingine na nyumba za Walimu kwa mchango wa nguvu za wananchi lakini bado tunahitaji msaada mkubwa kutoka kwa wananchi,wadau wa elimu na Serikalini."

Katibu wa Elimu, Uchumi, Malezi na mazingira wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Chunya, Philipo Mulugo anasema mazingira ya Iboma yanatia uchungu.

"Mazingira ya shule ya Iboma yanatia uchungu sana kwani serikali kupitia ilani ya CCM inapaswa kuliangalia hili na sisi kama viongozi wa chama na wadau wa elimu tunatakiwa kulipokea kwa masikitiko ikiwa ni pamoja na kushiriki kwa kuisaidia serikali katika ujenzi wa shule hii ya Iboma," anasema

"Sidhani kama kuna mtu ambaye atasikia taarifa ya mazingira ya shule ya Iboma ataamua kukaa kimya, basi huyo atakuwa siyo mpenda maendeleo ya elimu na mimi nitakwenda huko kama katibu wa elimu na nitapeleka mifuko ya saruji 10 ili iweze kuwasaidia,"anasema

Mulugo ametoa wito kwa wanachi wa Iboma na wale wa kata ya Kapalala wanaoishi nje kujitoa kwa hali na mali ili kuisaidia shule hiyo kuwanusuru wanafunzi kusoma chini ya mbuyu ili waweze kupata elimu bora.

Lakini Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Chunya Maurus Sapanjo amesema kuwa haifahamu hiyo shule na hajawahi kufika katika shule hiyo.

"Kwa kweli lazima niwe mkweli na muwazi siifahamu hiyo shule na wala afisa elimu wangu hajawahi kunipa taarifa ya shule hiyo kwamba kuna shule ina darasa moja na wanafunzi wanasoma chini ya mti wa mbuyu. Ndiyo kwanza nimeisikia kupitia gazeti la Mwananchi na imenisikitisha sana kuona katika wilaya yangu kuna shule yenye matatizo kama haya,"anasema.

Sapanjo anasema kuwa siyo nia yake na hajafurahishwa na taarifa hizo kwani malengo yake ni kuhakikisha baada ya miaka 10 watoto wa wilaya ya Chunya wanafika vyuo vikuu.

Anasema angekuwa anaijua shule hiyo asingekimbilia kujenga shule za sekondari za kata 18 wakati kuna shule ya msingi ina darasa moja na wanafunzi wanasomea chini ya mti wa mbuyu.

"Nimemwagiza afisa elimu wangu pamoja idara nzima ya elimu kuhamia shuleni hapo na kuhakikisha madarasa yanajengwa kwa haraka ili kuondokana na adha hiyo," anasema juu ya hatua alizochukua.

Kuhusu wanafunzi kujishughulisha na uvuvi wa samaki badala ya masomo, amesema msako mkali unafanyika kuhakikisha watoto wote wanarudi shuleni haraka na kuwachukulia hatua za kisheria wazazi wote watakaobainika wanashiriki katika kuwaruhusu watoto wao kufanya kazi ya vibarua ya uvuvi wa samaki na shughuli nyingine ziwani.

Mtikisiko wazuka Baraza la Mawaziri

Mwandishi Wetu
Raia Mwema

Novemba 25, 2009

  • Kikwete yaanza kumshinda
  • Sasa hata Dk. Shein azoza

SIKU chache tu baada ya kutuma ujumbe kwamba akipita mwakani hatabeba mawaziri wazee, Rais Jakaya Kikwete ameanza kutekeleza azma hiyo kwa kuwatangazia mawaziri wake kwamba amechoshwa nao kwa kuwa hawamsaidii, imefahamika.

Habari ambazo Raia Mwema imepata zinasema kwamba Rais Kikwete na hata wasaidizi wake, Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wamekuwa wakali isivyo kawaida yao katika vikao vyao vya kazi.

Kwa mujibu wa habari hizo, katika kipindi kiasi cha wiki mbili zilizopita, Rais Kikwete amekutana na mawaziri wake mara mbili na katika vikao hivyo amesema waziwazi kwamba mawaziri wake hawamsaidii kama alivyotarajia wakati akiwateua.

"Hakikua kikao cha baraza, lakini alizungumza kwa ukali akiwaambia kwamba alipowateua alikuwa na matumaini makubwa nao kwamba atakuwa amepunguza kwa kiasi kikubwa uzito wa kazi.

"Akawaambia amekuwa akilazimika kufanya mambo mengi ambayo yangeweza kufanywa na mawaziri wake aliowaamini na akawapa dhamana," anaeleza ofisa mmoja wa serikali aliyezungumza na Raia Mwema wiki kwa masharti ya kutotajwa gazetini.

Mtoa habari huyo amesema wiki iliyopita Rais Kikwete alikuwa mkali kwa wasaidizi wake kuliko ilivyopata kutokea tangu aingie madarakani mwishoni mwa mwaka 2005.

Imefahamika kwamba kabla ya kikao cha wiki iliyopita, kilichofanyika nje ya Dar es Salaam, Rais Kikwete aliwaita mawaziri wake ghafla katika hatua ambayo ilizua hofu miongoni mwao wakiamini kwamba huenda alitaka kuvunja Baraza lake.

Habari zaidi zinasema katika kikao cha awali waziri mmoja mwanamke alikwepa kuhudhuria baada ya kupata fununu kwamba Rais Kikwete alikuwa amekerwa na baadhi ya kauli zake za hivi karibuni.

Habari zinaeleza kwamba, hata Dk. Shein ambaye anafahamika ya kuwa mara nyingi hana hulka ya ukali amebadilika, na sasa naye ameanza kuwa mkali waziwazi katika vikao vya utendaji.

"Kuna kikao kimoja ambacho baada ya Rais kumbana waziri mmoja kutokana na kuwasilisha waraka uliokuwa umejaa mapungufu, Makamu naye alizungumza kwa ukali akimtaka waziri huyo kuacha kufanya mambo bila kufuata taratibu," anasema mtoa habari huyo.
















Rais Jakaya M. Kikwete

Anaongeza: " Katika kikao hicho Rais alimkatiza waziri huyo mara kwa mara akitaka ufafanuzi na wakati mwingine kumlazimisha waziri huyo kubadili baadhi ya mambo ambayo aliona yana makosa mengi katika waraka wake.”

Ukali wa ghafla wa Rais Kikwete, Dk. Shein na Pinda unatajwa kuwa umechochewa na utendaji usioridhisha wa mawaziri wengi unaosababisha viongozi hao wa juu kabisa kulazimika kufanya kazi ya ziada.

Katikati ya habari hizo ni hali kwamba mawaziri wengi wanashindwa kuitetea na kuisimamia Serikali ndani na nje ya Bunge, mbele ya umma na katika shutuma nyingi zinazotajwa kwenye vyombo vya habari. Anasema mtoa habari huyo: "Rais alieleza wazi kwamba anakerwa na taarifa za mara kwa mara katika vyombo vya habari zikionyesha udhaifu mkubwa wa Serikali yake huku wasaidizi wake wakiwamo mawaziri wakishindwa kutoa hoja zenye nguvu au mkakati mahususi wa kukabiliana na taarifa hizo.”

Japo tathmini inaonyesha kwamba si rahisi katika muda mfupi uliobaki kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu kuwa na mabadiliko katika Baraza la Mawaziri, Raia Mwema imearifiwa ya kuwa tayari mchakato umeanza ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa wa kuchunguza mienendo ya watu wakiwemo wajumbe wa sasa wa Baraza la Mawaziri na wajumbe watarajiwa ikibidi kufanyika kwa mabadiliko.

Habari zaidi zinaeleza kwamba yamekuwapo mapendekezo kwa Rais Kikwete ya kutaka abadili baadhi ya mawaziri waliopo kwa baadhi ya wabunge ambao wamekuwa wakitajwa kuwa wako msitari wa mbele katika inayotajwa kuwa ni vita ya ufisadi katika hatua ya kukisafisha Chama cha Mapinduzi (CCM) katika tuhuma za ufisadi na migawanyiko ya dhahiri ili kuvutia kura katika uchaguzi wa mwakani.

Mbali ya kuingiza sura mpya na kupunguza baadhi ya mawaziri, kuna taarifa kuwa yapo mapendekezo kwa Rais ya uwezekano wa kupandisha ngazi naibu mawaziri walioonyesha uwezo mkubwa.

Haya yakiendelea zimekuwapo taarifa za wizara mbalimbali ambako wafanyakazi wanawalalalimikia mawaziri wao kwa utendaji kazi usioridhisha.

Kati ya waliotajwa na wafanyakazi hao ni pamoja na Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, John Chiligati; Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na Naibu wake, Dk. Makongoro Mahanga; Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Sophia Simba.

Lakini akizungumza na Raia Mwema wiki iliyopita Chiligati alisema “hawezi kufanya mtihani na kujisahihishia mwenyewe.”

“Hayo maoni ya watu siwezi kuyaingilia, mimi siwezi kufanya mtihani na kujisahihisha mwenyewe lakini naamini watendaji ofisi wanajua naingia ofisini saa ngapi na natoka saa ngapi,” alisema Chiligati na alipoulizwa kuhusu shughuli za chama kuingilia majukumu ya serikali, alisisitiza kutotaka kujisahihishia mtihani.

Katikati ya mwezi huu akizungumza na vijana wa kutoka nchi mbalimbali za Afrika mjini Dar es Salaam, Rais Kikwete alituma salamu za mwanzo kwa wateule wake kwa kuwaambia vijana hao ya kuwa endapo atajaliwa kuongoza tena Tanzania mwakani, atafanya jitihada kubwa kuondokana na sura za wazee ambao atawabadilisha na vijana.

Akizungumza katika mkutano wa vijana hao wa kulea viongozi wa Afrika, Rais Kikwete alisema atafanya mabadiliko makubwa kwenye Serikali yake akshinda uchaguzi ujao.

Alisema Kikwete: “Wale viongozi wa rika langu, lazima waanze kuwaachia nafasi vijana. Tunahitaji wakuu wa wilaya vijana zaidi, wakuu wa mikoa vijana zaidi na hata mawaziri vijana zaidi. Ndivyo ilivyotokea kwetu sisi wakati tukiwa vijana.”

Mheshimiwa Rais Kikwete na first Lady wakitalii huko Jamaica


Rais Jakaya na mkewe Salma wakibembea hewani kutalii vivutio nchini Jamaica pamoja na Waziri wa Utalii nchini humo,Edmund Barlett (kulia) na Horace Clarke, mmiliki wa bembea hilo lipitalo meta 50 hewani umbali wa kilometa mbili.

Wednesday, November 25, 2009

Mabadiliko huja kwa dhamira ya kweli ya Kutekeleza Ahadi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jakaya Mrisho Kikwete.
Sijui kama kweli tunataka mabadiliko au tunaombea mabadiliko yatokee. Sijui kama tunafanya ili kusababisha mabadiliko au tunasubiri wengine wafanye ili tufurahie mabadiliko; Sijui hata kama tunajua vizuri ni mabadiliko gani hasa tunayataka na kama tunataka ni juhudi gani tumezifanya kushiriki kwenye mchakato wa kuleta mabadiliko hayo.


Tunaweza kubishana vijiweni na kwenye mitandao na kujaribu kubadilishana mawazo mchana kutwa na usiku kucha lakini mabadiliko hayaji kwa kusema. Mabadiliko hayaji kwa kupigiwa magoti au kwa kukemea giza usiku. Mabadiliko husababishwa na kutekelezwa.

Tukijifunza kwenye kampeni ya Obama utaona kuwa Wamarekani hawakuombea tu kuwa kiongozi mzuri au wamtakaye aje na alipojitokeza hawakukaa pembeni kuombea kuwa afanye vizuri ili hatimaye "alete mabadiliko" wanayoyataka. Wamarekani walishirikishwa katika kampeni kuanzia kuchangia fedha, muda wao, vipaji vyao n.k

Je kwanini tunafikiri sisi Tanzania tutapata mabadiliko kwa kubishana vijiweni na kwenye mitandao na kuoneshana nani anajua nini na anahusika na nini? Mabadiliko ndugu zangu hayaji kwa kunuia au kuwa "kusudio zuri" au kwa kujua ufisadi ulivyo mbaya na fisadi ni nani!!

Mabadiliko huletwa na watu waliokusudia kuleta mabadiliko hayo.

Je una mawazo yoyote kuhusu kushiriki katika mabadiliko tunayoyataka au kutoa mchango wa aina yoyote?

Niandikie utupe mawazo yako.

kyelacommunity@live.com

Huu si wakati wa Kukata tamaa



Mbunge wa Kyela Dk. Harrison Mwakyembe

Bila ya shaka mlolongo wa matukio kadha wa kadha yanaweza kumfanya mtu yeyote kushika tama na kukata tamaa. Hasa inapotokea matukio ambayo yanaihusu familia zetu, jamii zetu, au nchi yetu. Msururu wa kashfa ambazo zimeiandama nchi na viongozi wetu bila ya shaka vinaweza kukufanya ujisikie mpweke na mnyonge na zaidi kuweza kujiuliza "Tanzania ina matatizo gani?".

Kwa wengine kujiuliza swali hili kunaendana na hisia ya kuachwa peke (abandonment) na kukata tamaa (despair). Na zaidi ya yote kuna wengine ambao wanaweza kujihisi kuvunjwa moyo (discouraged) na hivyo kuona kuwa hakuna lolote na chochote kinachoweza kufanyika Tanzania ambacho kinaweza kuturudisha kwenye matumaini?

Je huu ndio wakati wa kukata tamaa na kuwaachia mafisadi wafanye wapendavyo? Je huu ndio wakati wa kukubali viongozi wabovu na wasio na uwezo alimradi tuendelee katika hali ya utulivu, amani na mshikamano? Je huu ni wakati wa kusalimu amri na kukubali kile ambacho kimetuangukia na kuwa yote ni "mapenzi ya Mungu"?

Je unajihisi kukata tamaa ukiangalia mambo yanayoendelea katika nchi yetu?

Niandikie:

Tabia za Watoto zinatokana na Makuzi.

Na Africar T Kagema




Makuzi ya mtoto yanaweza kugawanywa katika nyanja kadhaa mfano makuzi ya kimiwili, kiakili, kimaono,kimaadili n.k. Katika makala hii tutajaribu kuona jinzi marafiki wanavyoweza kuathri ukuaji wa mtoto kimaadili. Upo msemo kuwa tabia ya mtu inaweza kueleweka vyema kwa kuzingatia tabia ya rafiki yake au marafiki zake. Msemo huu unatilia mkazo dhana nzima ya kuchagua marafiki wema ili kujenga tabia njema.

Malezi ya mtoto huanzia nyumbani kwa wazazi wake. Kipindi cha awali cha maisha ya mtoto (miaka 0-2) mtoto huishi zaidi katika mazingira ya nyumbani na tabia zake zote hutegemea tabia za watu wa nyumba husika. Baada ya hapo mtoto huanza kutoka na kuchanganyika na watoto wa nyumba jirani pamoja na watu wa vimo tofauti na yake.

Pia kwa hali ilivyo sasa watoto huanza kwenda shule za awali au madrasa (miaka 3-6). Baadaye hujiunga na shule za msingi kuanzia miaka 7 - 14 na hatimaye kuingia sekondari akiwa na umri wa miaka 15-19. Tutaona kuwa umahiri wa stadi mbalimbali kama lugha, michezo,hobi na mengineyo hupatikana katika kipindi ambacho mtoto ameshaanza kuwa na maingiliano na watu wa nje ya familia yake.

Tutakubaliana kuwa wazazi kama waalimu wa mwanzo kabisa wa motto (Nursery Teachers) watahusika sana na mustakabali mzima wa tabia za mtoto wako. Hawa ndiyo wenye jukumu ya kumjengea msingi mzuri wa maadili ya jamii ambapo chimbuko la tabia njema hupimwa kutokana na jinsi mtu anavyoweza kutenda mambo yake kwa kuzingatia maadili ya jamii husika.

Katika nyumba ambayo maadili huchungwa watoto hujifunza pia kuchunga maadili. Marafiki katika familia hizi hulingana kabisa na familia husika katika suala zima la kuzingatia maadili.

Utakapofika wakati wa mtoto kutoka nyumbani na kuingia mitaani tayari kuwa amejengewa msingi ambao utamsaidia kupata marafiki wema. Awali wazazi humsaidia mtoto kuchagua marafiki ambao huwa ni wale wanaotoka katika familia zenye maadili mema.

Msingi huu pia humsaidia mtoto kuchagua hobi nzuri ambazo haziendi kinyume na maadili ya jamii. Izingatiwe kuwa tabia za wizi, uvutaji wa bangi, madawa ya kulevya, utoro shuleni n.k. huigwa na watoto wakiwa katika vikundi. Kama wazazi watawaacha watoto wao bila kuwapa muongozo bora wa namna ya kupata marafiki wema basi wasishangae watoto wao kukosa kabisa makuzi mema katika hii nyanja ya maadili na hivyo kuishia kuwa watu mizigo "liability" katika jamii.

Hivyo natoa wito kwa wazazi kukaa na watoto wao bila kuchoka kung’amua mabadiliko ya tabia zao ili waweze kuzibadilisha mapema kabla hazijazoeleka na kuonekana ni kitu cha kawaida kwao. Ni vema pia kufuatilia mafundisho wanayopewa watoto wawapo shule za awali ili kutambua maadili yanayoizunguka shule hiyo na kuchukua hatua mapema.

Kanisa au Misikiti ni sehemu muhimu sana kwa watoto kuhamasishwa kuhudhuria ili waweze kujifunza maadili ya Mungu. Watoto wanaoshindwa kuhudhuria makanisani au Misikitini huwa wanakosa mengi kwani zile ni sehemu zinazofundisha watoto maadili mema katika jamii. Vipindi kama vya Sunday School kwa wakristo na madrassa kwa waislam ni vipindi vizuri sana katika maadili ya watoto katika umri wao mdogo.

Watoto wakalishwe chini na waelezwe kipi cha kufanya na wakati gani, na kipi cha kutofanya na katika mazingira gabi. Wazazi wasipuuzie na kuacha tabia mbaya za watoto zikiendelea kukomaa, kwani kwa kufanya hivyo kutasababisha kushindwa kuwarekebisha mara wakiachwa na tabia zao. Kama wazee wasemavyo ‘’mkunje samaki angali mbichi’’, kwani akikauka (akikomaa awezi kufunzika tena).

Watoto wadogo wanahitaji watu wazima ili waweze kuwaongoza na kuwasaidia ili wajifunze tabia na maadili yanayokubalika na yale yasiyokubalika. Wanahitaji pia watu wa kuwasaidia ili wajifunze namna ya kushirikiana na wengine. Jinsi tunavyotoa muongozo wa namna hii inategemea malengo yetu kwa watoto tunaowafundisha, tunataka watoto hawa wawe watu wa aina gani? Je wawe na nidhamu ya woga na kutojiamini au wafundishwe tabia ya kutegemeana na yale yanayokubalika na yasiyokubalika.

Kumuongoza mtoto kunahitaji muda na uvumilivu, ni jambo muhimu sana iwapo mzazi anatumia muda fulani katika kuchunguza tabia na mwenendo na kujitahidi kurekebisha kwa upole. Hasira na ukali havisaidii; kama maji yazimavyo moto, upole hurekebisha tabia ya mtoto haraka sana. Tukumbuke pia watoto ni wanafunzi siku zote, wanahitaji uzoefu kutoka kwetu. Ni juu yetu basi kuwapa kilicho bora na muhimu katika uanafunzi wao.

Kawambwa ahimiza ujenzi wa Kiwanja cha ndege Songwe

na Gordon Kalulunga, Mbeya


WAZIRI wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawambwa, amehamasisha ukamilishaji wa Kiwanja cha Ndege cha Songwe, kilichopo mkoani Mbeya, baada ya kutembelea uwanja huo na kuukagua, kisha kuzungumza na mkandarasi na mhandisi mshauri wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini uwanjani hapo.

Kawambwa alitembelea na kuukagua uwanja huo juzi na kuwahimiza Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mkandarasi Kampuni ya Kundan Singh Construction Ltd ya nchini Kenya na mhandisi mshauri kutoka Falme za Kiarabu kuhakikisha ujenzi wa uwanja huo unakamilika mapema iwezekanavyo.

Waziri huyo alisema kuwa kwa sababu awali kikwazo cha uendelezaji wa ujenzi wa uwanja huo kilikuwa ni kutolipwa malipo ya awali mkandarasi anayejenga uwanja huo, lakini kwa sasa tayari serikali imekwisha kulipa deni hilo, hivyo hatarajii kuendelea kusuasua kwa ujenzi katika kiwanja hicho.

“'Kwa sababu serikali imelipa fedha zote za malipo ya awali kwa mkandarasi, hivyo hatutarajii kuona ujenzi wa uwanja huu ukisuasua kama mwanzo, maana kikwazo kilikuwa ni fedha,”' alisema Waziri Kawambwa.

Aidha, alifafanua kuwa ifikapo Januari mwaka 2010 anatarajia kupata taarifa nzuri zaidi za maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambao ni tegemeo kubwa la wananchi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini na taifa kwa ujumla.

“'Kwa kipindi cha mwaka wa bajeti 2008/2009 serikali imetenga sh bilioni 18 kwa ajili ya umaliziaji wa ujenzi wa kiwanja hiki ambacho kina umuhimu sana kwa taifa letu, hivyo ni muhimi pia nanyi kama wataalamu mkaona kuwa ni jinsi gani serikali ilivyoupa kipaumbele uwanja huu,” alisema Kawambwa kwa matumaini ya kumalizika kwa uwanja huo kama matarajio ya serikali yalivyo.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa kiwanja hicho mbele ya Waziri huyo wa Miundombinu kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Prosper Tesha, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi na Uhandisi, White Majula, alisema mkandarasi tayari amemaliza kukata na kujaza udongo njia za kuruka na kutua ndege ambazo waziri alizitembelea na kuzikagua.

“Maeneo yote ya usalama katika njia ya kuruka na kutua ndege yenye urefu wa mita 1,800 tayari mkandarasi ameyakamilisha kwa asilimia 65 na amekamilisha kazi ya ufungaji wa mitambo ya kusaga mawe kwa ajili ya kokoto na ameanza kufunga mtambo wa lami,” alisema Majula.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya uhakika vya habari, imeelezwa kuwa kampuni hiyo kutoka Falme za Kiarabu tayari imelipwa shilingi bilioni 3.1, ambapo kiwango hicho cha fedha kinajumuisha gharama za kazi za kufanya marejeo ya usanifu wa njia za kuruka na kutua ndege pia usimamizi wa utekelezaji wa ujenzi unaoendelea.

Kandarasi ya kumalizia kazi za ujenzi wa kiwanja hicho cha Songwe ilisainiwa Septemba 12 mwaka 2008 na kukabidhiwa Oktoba 19, mwaka huo huo, inatakiwa kazi hiyo ikamilike kwa kipindi cha miezi 18 kwa gharama ya sh bilioni 32.

Tuesday, November 24, 2009

Ufisadi chanzo cha wananchi kupoteza imani kwa CCM

NA MWANDISHI WETU
















Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Yusuf Makamba.

Watanzania wanasifika katika bara la Afrika kwa uvumilivu wao hata nyakati zisizoweza kuvumilika. Dhana hii inaweza kuwa ni matunda aliyotuachia Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Dalili za uvumilivu zinaonekaka wakati wa Utawala wa Serikali ya awamu ya nne. Serikali na viongozi wake wamekuwa wanaendesha serikali kinyemela kana kwamba haikuchaguliwa na wananchi.

Mdororo wa uchumi haukuanza leo katika dunia hii. Tofauti ya mdororo wa uchumi unaotuathiri sasa ni kwamba una miale mikali kuliko midororo ya uchumi iliyopita.

Ni katika mvurugano huu wa uchumi, Watanzania walitegemea kwamba viongozi waliowachagua na hatimaye kuunda serikali wangetafuta mbinu mbadala ili kulinasua Taifa na watu wake ili miale ya mdororo wa uchumi uliopo usingewaumiza sana. Matokeo yake ni kwamba wanaongeza joto la miale na waathirika wa miale hiyo ni Watanzania asilimia 85 waliotopea katika ufukara ndio wanaoumia kwenye joto la mdororo huo.

Wizi uliojitokeza na unaofanywa na vigogo wa Serikali ya CCM ni dalili fika zinazoonyesha kuwa maadili na itikadi iliyozoeleka ya CCM vyote hivyo vimewekwa kando.

Watuhumiwa wote wa wizi wa fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ni vigogo wa CCM na wale wa serikali yake.

Katika orodha hiyo ya watuhimiwa hakuna hata mwananchi mmoja aliye fukara ametuhumiwa na wala hakuna hata mwanachama mmoja wa vyama vya upinzani amediriki kujihusisha na ufisadi.

Ufisadi wote unaozungumzwa ni wa viongozi wa serikali ambao wamefikishwa mahakamani jambo ambalo Watanzania wanaona ni mchezo wa kuigiza.

Watanzania wanaona ni mchezo wa kuigiza kwa sababu vigogo wote waliofikishwa mahakamani ukijumulisha kile kinachodaiwa wameiba haifiki sh. bilioni 133. Hapa panajitokeza swali ambalo halina majibu kwamba hao wengine ambao wanatuhumiwa kinadharia tu watafikishwa lini mahakamani?

Tanzania inashuhudia amani ya mioyo tuliyorithi kutoka kwa Mwalimu Nyerere imetoweka kabisa. Watanzania wanapozungumza amani sio lazima zilie bunduki.

Ukosefu wa amani ni pamoja na kukosa mitaji, kukosa milo mitatu kutwa, dhuluma, rushwa na ufisadi vikiwa mstari wa mbele kuzidi nchi zote zilizo chini ya jangwa la Sahara.

Kukosekana kwa ajira, kuongezeka kwa ujambazi na ujangili si dalili nzuri ya kudumisha amani katika Taifa. Matatizo haya yote yalipaswa kurekebishwa na serikali.

Viongozi wetu wakiwa chini ya mwamvuli wa Rais Jakaya Kikwete hawaonekani kukemea maovu haya ambayo Watanzania hawakuzoe kuwa nayo.

Wazee wetu kama Peter Kisumo, Pancrasi Ndejembi, Joseph Butiku, Mohamed Raza, John Malecela, wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam na Waandishi maarufu kama Jenerali Ulimwengu wao wamekuwa wanayavalia njuga maovu yote yanayovurundwa na viongozi wetu kwa bahati mbaya serikali na chama chake imekuwa haitoi msisitizo ili kuafikiana na mawazo hawa.

Kwa mfumo huu wa falsafa na siasa ambazo ni za nadharia tu zimekuwa hazina tija kwa Watanzania. Hotuba za majukwaani zimekuwa haziendani na vitendo na hatimaye kudumaza usalama katika nchi na kuwaacha Watanzania wakijiuliza, wanakokwenda.

Suala zima katika Taifa ni kwamba nchi haina amani kwa sababu, wananchi hawana mlo uliokamilika, mafukara wa kutupwa wakati viongozi wao wanajinafasi kana kwamba wako mbinguni, usalama majumbani umekuwa haupo kwa sababu ya ujambazi uliokirithiri na polisi ina vitendea kazi duni ukifananisha na silaha zilizomo mikoni mwa majambazi.

Tatizo jingine Taifa halijaongeza ajira kwa polisi. Polisi tuliyonayo sasa ni ileile aliyotuachia Mwalimu Nyerere.

Kukosekana kwa utawala bora katika Taifa kumeathiri sana suala zima la usalama katika nchi. Watendaji wa tarafa, mitaa, vitongoji na kata wamekuwa tishio kubwa kwa usalama wa Raia.

Watendaji hawa wanajiita watunza usalama madaraka ambayo hata katika Katiba ya nchi hayapo. Kwa mshangao wa Watanzania wengi watendaji wamekuwa wanachukua sheria mikononi huku wakijua sio stahili yao, lakini wakuu wa mikoa na wilaya licha ya kushindwa kukemea, wamekuwa hawawachukulii sheria za nidhamu hivyo kuhalalisha vitendo vibaya vinavyofanywa na watendaji hao. Ukosefu wa utawala bora na sheria katika Taifa ndio umehatarisha usalama wa nchi.

Dhana ya kudumisha demokrasia endelevu katika Taifa haipo. Serikali pamoja na CCM kama alivyosema Rais Kikwete wakati wa kuadhimisha miaka kumi ya kifo cha Mwalimu Nyerere ni kwamba viongozi wameacha kabisa kusikiliza kero za wananchi na kuwasaidia.

Kinachobaki sasa ni porojo nyingi za siasa zisizokuwa na tija na kujilimbikizia mali ili kuja kugombea uongozi mwaka 2010.

Wanasiasa wengi wamebadili dira na maendeleo ya kisiasa na hatima yake wamegeuza siasa mradi wa kujinufaisha wao na familia zao.

Kwa sababu wakati wanagombea hivyo vyeo vya siasa wanatumia rushwa kwa hiyo wakivipata wanahakikisha fedha yao yote iliyotumika katika rushwa inarudishwa kwa nyakati mbalimbali. Hii ina maana kwamba, maendeleo ya wapiga kura yanawekwa pembeni.

Watanzania ambao kusema kweli wamechoshwa na siasa za CCM zenye poroja nyingi na zisizokuwa na tija. Ili wajinasue kutoka kwenye matatizo hayo wanadhani ni wakati muafaka wa kukiweka Chama Cha Mapinduzi na watafute ustarabu mwingine ambao pengine unaweza ukaleta neema ambayo itawanufaisha wao na vizazi vijavyo.

Suala ni kwamba Siasa za Tanu na CCM zimekuwa katika Tanzania kwa miaka 48 bila maendeleo yoyote kwa wananchi.

Tutaboreshaje elimu katika shule za serikali?

BY BENJAMIN NKONYA

Chimbuko la maendeleo ya elimu nchini ni matokeo ya michakato ya sheria, falsafa na sera zilizoanzishwa katika vipindi mbalimbali kabla na baada ya uhuru. Baada tu ya kupatikana uhuru mwaka 1961, serikali ilitunga sheria ya elimu namba 83 ya mwaka 1962 iliyofuta sheria ya elimu ya mwaka 1927 ambayo iliruhusu utoaji wa elimu na mafunzo kwa mfumo wa ubaguzi wa rangi, dini na makabila.

Katika sheria hii, serikali iliekeza mitaala, uongozi na ugharamiaji wa elimu na mafunzo ufuate usawa. Azimio la Arusha la mwaka 1967 lilianzisha falsafa ya elimu ya kujitegemea ambayo ilisababisha mabadiliko makubwa katika sera za jumla za kijamii na kiuchumi.

Falsafa hii, ambayo iliasisiwa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ndiyo inaweka dira katika mfumo wetu wa elimu hadi leo, inaweka mkazo katika kuondoa matabaka kwenye utoaji wa elimu, utengano (alienation) kati ya shule na jamii na kusaidia kuondoa kasumba ya wasomi ya kujibagua na kutumia elimu waliyoipata kwa manufaa yao binafsi.

Aidha falsafa hii inaelekeza katika kuunganisha nadharia na vitendo, kwa dhana kuwa elimu isipatikane vitabuni tu bali ijumuishe na ile ipatikanayo kutokana na uzoefu wa kutenda au kufanya kazi ya kuongeza tija.

Ili kuhakikisha kwamba haya yanafikiwa na pia kuhakikisha kwamba wanafunzi wanawajibika na upatikanaji wa mahitaji yao, falsafa hii inaelekeza shule kuwa vituo vya kuzalisha mali ili kuchangia gharama za uendeshaji kwa asilimia ishirini na tano. Pia elimu inayotolewa katika ngazi zote iwe na maarifa na stadi za kumwezesha mhitimu kuishi na kufanya kazi yenye manufaa katika jamii.

Katika kutekeleza falsafa hii, shule karibu zote zilitaifishwa na kuendeshwa na serikali kuanzia mwaka 1967. Ili kuondoa aina zote za ubaguzi, serikali ilikubali kugharamia elimu katika ngazi zote. Pamoja na hayo, kila shule ilianzisha mashamba ambayo yalikuwa maarufu kama mashamba ya elimu ya kujitegemea. Hali hii ilimfanya mwanafunzi wa Kitanzania kuwa tayari kujitegemea mara tu baada ya kuhitimu mafunzo ya elimu ya msingi. Kwa hakika falsafa hii ilishabikiwa sana na kila Mtanzania.

Pamoja na uzuri wa falsafa hii, kuna changamoto zilizoukabili mfumo mzima wa elimu katika miaka kumi ya utekelezaji wa falsafa hii. Kama wote tunavyofahamu, katika nusu ya pili ya miaka ya 1970, ubora wa elimu yetu ulishuka sana kiasi kwamba serikali iliruhusu walimu wasio na sifa kuanza kufundisha katika shule za msingi.

Changamoto hii iliambatana na ukosefu wa zana za kufundishia na kujifunzia kama vitabu, maabara, maktaba n.k. Sambamba na changamoto hii, ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi halikuenda sambamba na ongezeko la idadi ya vyumba vya madarasa na samani zake, achlia mbali nyumba za waalimu.

Hivyo ililazimu chumba kimoja cha darasa kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi kuliko idadi inayomfanya mwalimu alimudu darasa kiufundishaji. Pamoja na changamoto hizo, hata suala la usimamizi wa elimu nalo lilikuwa gumu kutokana na shule kuwa nyingi katika mtawanyiko wa kijiografia ambao una ufanisi mdogo. Matokeo ya hali hii ilikuwa ni kushuka kwa elimu kwa haraka sana.

Serikali iling’amua changamoto hizi na kutafuta namna ya kuziondoa ili elimu iendelee kutolewa kwa ubora unaotegemewa. Mwaka 1978 Bunge lilitunga sheria mpya ya elimu namba 25 ambayo, pamoja na mambo mengine, iliruhusu watu binafsi, mashirika ya dini, asasi za kiraia na makampuni kuanzisha, kusajili na kuendesha shule.

Kuanzishwa kwa sheria hii kulianza kuonyesha matumaini ya kunusuru ubora wa elimu kwani shule nyingi binafsi zilionyesha mafanikio. Kuna changamoto kadhaa ambazo zilijitokeza katika miaka kumi na tano ya kwanza ya utekelezaji wa sheria hii.

Changamoto hizi zilirekebishwa kupitia sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995. Hivyo mfumo wetu wa sasa wa utoaji wa elimu na mafunzo nchini unaongozwa na sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995 (iliyopata nguvu kutokana na marekebisho ya sheria ya elimu Na. 25 ya mwaka 1978 iliyorekebishwa kwa sheria Na. 10 ya mwaka 1995), sera ya elimu ya ufundi ya mwaka 1996 na sera ya elimu ya juu ya mwaka 1999.

Pamoja na ukweli kwamba shule za serikali zinaendeshwa kwa kodi za Watanzania pamoja na ufadhili mwingi sana kutoka mashirika mbalimbali ya ndani nje ya nchi, elimu yetu, hasa inayotolewa na shule za serikali, bado ina changamoto nyingi sana katika viashiria vya utoaji (input), mchakato (process) na matokeo (outputs).

Baada ya marekebisho hayo na baada ya sekta binafsi kujiimarisha ipasavyo, Watanzania wameendelea kushuhudia kukua kwa haraka sana kwa elimu katika sekta binafsi licha ya ukweli kwamba shule hizi hazina ruzuku yoyote kutoka serikalini. Sasa ni zaidi ya miaka thelathini tangu kuruhusiwa kwa sekta binafsi kuingia katika utoaji wa elimu.

Pengine ingekuwa busara kudurusu sababu hasa za tofauti hizi na kutafuta namna ambavyo elimu yetu katika sekta ya umma inaweza kuboreshwa.

Ni ukweli usionpingika kwamba gharama za uendeshaji katika shule za serikali ni kubwa kuliko gharama katikashule binafsi. Hii inatokana na ukweli wa kiuchumi kwamba kadri mradi unavyozidi kuwa mkubwa ndivyo ufanisi kwa kila shilingi inayotumika unavyozidi kushuka. Hali hii inakabili vilivyo shule zetu za serikali.

Moja ya viashiria vya kushuka kwa ufanisi ni hii hali ya waalimu kuwa na malalamiko yasiyoisha kuhusu mapunjo wanayopata katika malipo yao, baadhi ya wanafunzi kuvuka madarasa na vidato bila kujua kusoma na kuandika, kukosekana kwa maabara, maktaba, vitabu na vifaa vingine vya kujifunzia na kufundishia na mambo mengine yanayofanana na hayo.

Sababu nyingine za kudorora kwa elimu katika shule za serikali ni kuingiliwa kupita kiasi na wanasiasa. Utakuta taarifa ya wakaguzi inaonyesha kabisa kwamba shule fulani haitakiwi kusajiliwa kutokana na kutotimiza baadhi ya vigezo vya usajili. Pamoja na taarifa hizo, utakuta mwanasiasa anaingilia kati na kulazimisha shule hiyo isajiliwe.

Hivyo hata uendeshaji wake huenda kisiasa siasa tu bila kujali vigezo muhimu vya uendeshaji wa shule. Utakuta shule ya serikali imesajiliwa lakini haina hata kitabu kimoja wala maabara. Itakuwa ni ajabu isiyo kifani kukuta shule kama hii ikitoa elimu bora.

Hali ni tofauti kabisa katika shule binafsi. Shule hizi husimamiwa na kwa ukaribu sana. Shule hizi hukaguliwa na kusajiliwa baada ya kutimiza vigezo vyote vya usajili. Huwezi kukuta shule binafsi inasajiliwa wakati haina maktaba yenye vitabu au maabara zenye vifaa vyote. Hata baada ya usajili, wakaguzi hufika katika shule hizi mara kwa mara kuangalia kama kila kigezo cha utoaji wa elimu kinazingatiwa.

Sambamba na hili, utakuta mmiliki wa shule hizi anafuatilia kwa karibu sana kila kinachoendelea shuleni na kuhakikisha wanafunzi wake wanapata huduma zinazotakiwa.

Kwaujumla wake ni kwamba shule binafsi huendeshwa kwa kufuata mahitaji ya wateja wake na kutimiza masharti yote yanayowekwa na serikali.

Kurunzi haioni kama itatosha tu kukosoa bila kutoa mapendekezo ya ubereshaji. Njia ya kwanza ni kuondoa siasa katika uendeshajiwa usajili na uendeshaji wa shule.

Hii inaweza kufikiwa kwa njia ya kuifanya idara ya ukaguzi kuwa wakala inayojitegema badala ya hali iliyopo ya kuwa idara katika Wizara Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Itakuwa ni ajabu ya ngariba kujitia suna mwenyewe kama kitengo hiki kitatenda haki hasa wakati shule ya serikali inapofanya makosa.

Njia ya pili ni kuweka ushirikiano kati ya wamiliki wa shule binafsi na serikali ili kuondoa tatizo la kushuka kwa ufanisi wa usimamizi unaotokana na kukua kwa idadi ya shule zinazosimamiwa na mmiliki mmoja.

Katika hali hii, mmiliki wa shule binafsi anaweza kuwekwa kuwa meneja wa shule ya serikali (hasa hizi za kata) iliyo karibu naye. Kama meneja, atahakikisha kwamba anashirikiana na bodi ya shule katika kuhakikisha kwamba shule hii ya kata inatoa elimu bora kama ilivyo shule yake.

Elimu ni mali ya umma na inatakiwa kugharamiwa na umma hata kama inatolewa na shule/chuo binafsi. Kurunzi inaamini kabisa kwamba, tukilizingatia hili, tutakuwa tumekata kabisa mizizi yote ya ufisadi dagaa, papa na nyangumi na tutakuwa tumeenzi na kuhuisha fikra sahihi za Baba yetu wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.