Tuesday, October 27, 2009

Urafiki wa Lowassa, JK usiingilie urais-Wabunge

*Selelii, Kimaro wataka afikishwe kortini
*Walaumu serikali kwa kutoa majibu ya ovyo
*Lowassa: Sizungumzi na vyombo vya habari

Waandishi Wetu, Dar, Dodoma

Majira26 October 2009

WAKATI mkutano wa bunge unaanza leo, mzimu wa mkataba tata wa Richmond umeendelea kumwandama aliyekuwa Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa baada ya baadhi ya wabunge kudai kuwa anastahili kuchukuliwa hatua zaidi ya ile ya kujiuzulu kutokana na kutajwa kwake katika kashfa hiyo.

Wabunge hao kwa nyakati tofauti wamesema kuwa urafiki ambao Bw. Lowassa alisema upo baina yake na Rais Jakaya Kikiwete usiingilie urais, serikali na uiachwe ifanye kazi yake kwa kumchukulia hatua kutokana na kuliingizia taifa hasara.

Akizungumza na Majira kwa njia ya simu jana, Mbunge wa Nzega, Bw. Lucas Seleli Bw. Selelii alisema kutochukuliwa hatua za kisheria kwa Bw. Lowassa kunatokana na urafiki uliopo kati rais Kikwete na mbunge huyo wa Monduli.

Alisema Rais Kikwete anapaswa kuamua kusuka au kunyoa kwa kuacha urafiki na kufuata sheria za nchi kwa kumfikisha Bw. Lowassa katika vyombo vya sheria, kwani alionekana wazi kushiriki kupitisha mkataba huo tata.

"Tulipokuwa tukijadili taarifa ya Kamati Teule ya Bunge tulibaini kuwa bila shaka alishiriki katika uamuzi huo, hivyo tulimwambia apime akapima, akaamua kujiuzulu. Huu ulikuwa ni uamuzi wake binafsi lakini sisi hatukuishia hapo.

"Tuliacha na serikali nayo iamue nini cha kufanya lakini hadi sasa imekuwa ikitupatia majibu ya ovyo ovyo tu, tunajua hawa watu ni marafiki tangu muda mrefu lakini urafiki na urais ni kitu tofauti. Hapa ni kazi wanatakiwa kuweka urafiki pembeni na kuwatumikia wananchi," alisema Bw. Selelii.

Alisema kama kweli nchi inafuata sheria na utawala bora, serikali inatakiwa kumshtaki Bw. Lowassa kutokana na kosa alilofanya kwani limekuwa likiipotezea nchi pato kubwa hadi sasa.

Alisema kuwa sheria ni sawa na moto, kwa kuwa moto unaweza kuundaa mwenywe lakini ukakuunguza.

Alisema katika mkutano wa 17 unaoanza leo mjini Dodoma wamekamia kumaliza suala hilo na kuhakikisha kuwa sheria inachukuwa mkondo wake kwa kuwachukiliwa hatua watu wote walihusika katika mkataba huo tata.

Kauli ya Selilii imekuja siku moja baada ya gazeti moja kutoa vielelezo vinavyoonesha jinsi Bw. Lowassa alivyohusika kushinikiza kusainiwa kwa Mkataba wa Richnond.

Lakini Bw. Lowassa alipoulizwa hakuwa tayari kuzungumza na gazeti hili. "Sikusikia vizuri swali lako kwa kuwa simu inakatakata, lakini siko tayari kuzungumza na vyombo vya habari kwa sasa hadi hapo nitakapopanga," alisema Bw. Lowassa na kukata simu.

Mapema, Mbunge wa Vunjo, Bw. Aloyce Kimaro naye aliungana na Bw. Selelii, akisema kuwa Rais Kikiwete anatakiwa kuuweka pembeni urafiki wao na kuchukua uamuzi utakaowafurahisha wananchi waliomweka madarakani.

Alisema Rais anatakiwa kukumbuka kuwa madaraka aliyonayo ni ya milele na yanagharimiwa na wananchi, hivyo hatakiwi kufanya machezo kwa kuchanganya urafiki na madaraka hayo, kwani kutomchukulia hatua Bw. Lowassa ni sawa na kuwadharau wananchi anaowangoza.

"Iwapo atachukua uamuzi mzito wa kumfikisha Bw. Lowassa katika vyombo vya sheria utakuwa si uamuzi wake bali ni wa wananchi kwa kuwa cheo hicho si mali ya Lowassa au ya Kikwete bali ni mali ya wananchi," alisema Bw. Kimaro.

Alisema hadi sasa hajui ni kwa nini rais anakuwa mzito katika kutoa maamuzi katika jambo hilo kwani mapendekezo ya Kamati Teule ya Bunge na maoni ya wabunge yako wazi.

Mwansheria wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Tindu Lisu, alihoji, "Lowassa mwenye alishasema kuwa urafiki wake na Rais Kikwete haukuanzia barabarani, sasa kwenye mazingira ya aina hiyo anaweza kumshitaki?

"Mtu wa kumshitaki mahakamani ni DPP (Mwendesha Mashitaka wa Serikali) ambaye anachaguliwa na Rais, na rais ni rafiki yake Bw. Lowassa, sasa hatawezaje kumshitaki katika mazingira hayo." alihoji Bw Lissu.

Alisisitiza kuwa Rais akitaka anaweza kumfikisha, Bw. Lowassa, katika vyombo vya sheria kujibu mashitaka ya kutumia vibaya ofisi yake.

"Kuna ushahidi mkubwa unaoonesha jinsi Bw. Lowassa alivyohusika, ukisoma ripoti yote ya Dkt. Mwakyembe (Harrison) utaona inavyoeleza wazi jinsi alivyohusika...barua zipo nyingi zinazothibitisha alivyoshiriki," alisema na kuongeza kuwa;

"Lowassa ni rafiki wa karibu wa Rais Kikwete, bado ana nguvu serikalini ndiyo maana haguswi."Alisema hata makosa aliyofanya Bw. Lowassa yakifumbiwa macho lakini baadaye anaweza kushitakiwa. "Makosa yanayomkabili ni ya jinai ambayo hayafi hadi baada ya miaka 60," alisema na kufafanua kuwa hata serikali zijazo zinaweza kumfikisha mahakamani.

Akizungumza na Majira kwa njia ya simu aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza kashfa ya Richmond, Dkt. Mwakyembe alisema yeye kama mwenyekiti hawezi kusema lolote kuhusu taarifa hiyo bali anasubiri kile kitakachowasilishwa na serikali.

“Unajua mimi nilikuwa mwenyekiti wa kamati sasa siwezi kusema lolote, waache Wabunge wengine waseme, mimi nikisema inaweza kutafsiriwa vibaya kwa kuwa nilikuwa mwenyekiti,” alisema Dkt. Mwakyembe.

Kauli hizo za wabunge zimekuja wakati serikali inatarajia kuwasilisha taarifa yake ya utekelezaji ya maazimio 23 ya Bunge kuhusu Richmond muda wowote kuanzia leo.
__________________

No comments:

Post a Comment