Wednesday, October 28, 2009

Mwakyembe ataka Hosea asijihami

Tuesday, 27 October 2009 15:12

*Asema hawezi kuwaziba midomo wabunge
*Asisitiza chanzo ni kashfa ya Richmond

Na John Daniel, Dodoma

MBUNGE wa Kyela. Dkt. Harison Mwakyembe, (CCM), amemshukia Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzua na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Dkt. Edward Hosea na kumtaka aache mara moja kutafuta njia ya kujihami kwa kuwahoji ili kuwaziba midomo wabunge badala yake izingatie utawala wa sheria.

Dkt. Mwakyembe aliyeongoza Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza kashfa ya kampuni tata ya kuzalisha umeme wa dharura ya Richmond, na kumtuhumu Dkt. Hosea kwa kuisafisha, anaungana na mbunge wa Bumbuli, William Shelukindo kuhusisha kashfa hito na hatua ya TAKUKURU kuwahoji wabunge kuhusiana na posho wanazopokea.

Madai ya wabunge hao yamekuja wakati TAKUKURU ikiendelea kuwahoji baadhi ya wabunge ikiwatuhumu kupokea posho mara mbili kutoka serikalini na kwenye mashirika ya umma, huku wakiwa wameshalipwa na ofisi ya Bunge.

Tofauti na Bw. Shelukindo aliyekiri kuhojiwa na kutoa ushirikiano, Dkt. Mwakyembe ambaye kitaaluma ni mwanasheria amesema hawezi kukubali kuhojiwa na TAKUKURU kwa sasa hadi hapo serikali itakapomaliza kutekeleza maamizio 23 ya Kamati Teule ya Bunge, mojawapo likiitaka kumwajibisha Dkt. Hosea.

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Habari wa Bunge jana, Dkt. Mwakyembe alisema amesikitishwa na kitendo cha TAKUKURU kuwaita wabunge katika kundi kwa kuwapigia simu kuwahoji kuhusu malipo ya posho ya vikao mbalimbali hukutaasisi hiyo, nayo ikiwa inawalipa wabunge pale inapokutana nao Dar es Salaam.

“Leo nimesoma gazeti moja (Sio Majira) likiwa limeandika habari kwamba sijui Mwakyembe amechanganyikiwa, ameitwa na TAKUKURU ameomba hifadhi, kwanza hili ni gazeti la mafisadi na si mara ya kwanza kuandika habari kama hizi, gazeti hili linamilikiwa na mafisadi.

"Waandishi wa (hilo gazeti) wapo hapa, tuambieni Kagoda ni nani, Richmond ni nani, hili gazeti linamilikiwa na mafisadi na mnawajua, sina haja ya kuwataja na tulishawataja,” alisema.

Mbunge huyo aliongeza: “Lakini ninachotaka niseme ni kwamba kwa muda wa karibu mwezi sasa, TAKUKURU wamekuwa wakiwaita wabunge kwa makundi tena kwa kuwapigia simu, na mimi walinipigia simu nikiwa jimboni, nikakataa kwenda sasa huo ni ujasiri kwa sababu bado tunasubiri utekelezaji wa serikali kuhusu TAKUKURU katika suala la Richmond, hatujapata majibu hayo, huyo huyo anayetakiwa kushuguhulikiwa (Dkt. Hosea) anatuita eti kutuhoji,” alisema Dkt. Mwakyembe na kuongeza.

“Huo siyo utawala wa sheria, hili ni bunge la tisa lakini hata sisi tumekuta wabunge wakilipwa posho au kuandaliwa chakula, sisi tunawapokea mawaziri kila siku katika maeneo yetu hatujawahi kusema kwamba leo tusimwandalie chakula kwa kuwaamelipwa, hapana. Hata wao TAKUKURU wametuita pale Dar es Salaam walitulipa posho tena mpaka ya kulala, yapo masuala mazito ambayo tunataka TAKUKURU wawasaidie Watanzania si michezo michezo hii,” alisema.

Alisema fedha zinazotumika katika fungu hilo hupitishwa bungeni kila mwaka kwa jina la hospitality (takrima) na kwamba ni jambo la kawaida kumkarimia mgeni anapokutembelea na kwamba kama mtu hapendi kufanya hivyo halazimishwi lakini kuwahoji wabunge juu ya malipo hayo ni kutaka kuwaziba midomo ili wawe na hofu kuhoji utekelezaji wa serikali kuhusu mkuu wa TAKUKURU.

“Mimi waliniita na nimekataa kwenda sasa kama wana hoja waende mahakamani tutakutana huko na nitawaumbua huko,” alisema Dkt. Mwakyembe. Alisema yeye kama mbunge mwana taaluma ya sheria hawezi kukubali kuona watu wanatumia baadhi ya vyombo vya habari kuendelea kupotosha ukweli kwa maslahi yao na kuwaomba wanahabari kusaidia jamii kuelewa hoja za msingi za taifa badala ya baadhiyao kupotosha ukweli kwa maslahi yao.

“Eti mafisadi wanataka kuniangusha kule jimboni kwangu, najua leo kuna ndege imepeleka magazeti ya fulani Kyela na kugawa bure, lakini nawaambia wananchi ni waelewa, mafisadi kuning’oa Kyela itawabidi wao na wake zao wapige kambi na wahamie Kyela kwa miaka mitano,” alisema Dkt. Mwakyembe.

Kauli hizo za Dkt. Mwakyembe zimekuja siku mbili baada ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta kuishtumu TAKUKURU kupitia gazeti kuwa inadhalilisha wabunge kwa kuwahoji bila kufuata taratibu, ikiwamo kuifahamisha ofisi yake.

Lakini taasisi hiyo kwa upande wake inasema ilipata baraka za bunge kufanya hivyo na wabunge wanastahili kuitikia wito kwa kuwa hakuna mtu aliye juu ya sheria.

Malumbano hayo yanaendelea wakati Mkutano wa 17 wa Bunge unaotarajia kuhitimisha kashfa ya Richmond kwa serikali kueleza ilivyotekeleza maazimio 23 ya bunge ukiendelea.

No comments:

Post a Comment