Friday, October 23, 2009

Wapenda maendeleo tusaidieni- Paroko wa Kyela

Na Pd. Raphael Kilumanga, Mbeya

PAROKO wa Parokia ya Mtakatifu Mathias Mulumba, Kyela katika Jimbo Katoliki la Mbeya, amewapongeza waamini wake kwa kujitolea kutumia nguvu zao kujenga kanisa na akatoa wito kwa wenye mapenzi mema kuwaunga mkono kwa hali na mali kukamilisha ujenzi huo.

Paroko huyo Padre Paul Mwanyalila, alitoa pongezi na wito huo wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizi parokiani kwake juma lililopita.

Alisema moyo waliouonesha waamini wa parokia hiyo katika kujiletea maendeleo, hauna budi kuigwa na jamii nzima kwani mtu anayeonesha bidii mwenyewe ni rahisi kusaidiwa pale nguvu zake zinapoishia.

Alisema waamini hao wamechangia nguvukazi na mali zao kwa ujenzi wa kanisa ambalo kwa mujibu wa tathmini za mwaka 1996, linagharimu jumla ya shilingi milioni 146/= za Kitanzania.

"Gharama hiyo ilikuwa kwa kipindi hicho na ni wazi kwamba sasa zimepanda," alisema.

Alitoa wito kwa Serikali, makanisa, mashirika na asasi za kidini na za kibinafsi; pamoja na watu wote wenye mapenzi mema na hasa wazawa wa Kyela popote walipo, kuchangia kwa hali na mali ili kufanikisha ujenzi huo.

Parokia ya Mtakatifu Mathias Mulumba, Kyela, ina waamini takribani 6000 na vigango zaidi ya14. Ilianzishwa mwaka 1968.

Ujenzi huo utakapokamilika, kanisa hilo litamudu kuhudumia waamni 1200.

Serikali, asasi na wafadhili mbalimbali wamekuwa wakisisitiza jamii kuchangia kwa juhudi katika kujiletea maendeleo na huku wakisema wako tayari kuwasaidia pale ambapo juhudi za kujiletea maendeleo zimekwama badala ya kutaka watu kutaka kusaidiwa kila kitu.

Hivi sasa ujenzi huo uko kaika hatua za kukamilisha msingi na kunyanyua ukuta.
Kwa yeyote mwenye mapenzi mema aliyeguswa na ombi hili, na kupenda kuunga mkono juhudi za waamini hao, atume mchango au msaada wake kwa: Paroko,


Parokia ya Kyela,
S.L.P. 170.
KYELA.

No comments:

Post a Comment